Baada ya kupata pigo la aina yake jana kwa Mbunge wa Kilombero, Peter Lijuakali kuhukumiwa kifungo cha miezi sita jela, Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimeeleza kutorishwa na uamuzi huo.

Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Kilombero, Timothy Lyon alieleza kuwa mahakama hiyo ichukua uamuzi huo dhidi ya Lijuakali kama fundisho kwani alishakutwa na hatia katika kesi nyingine tatu za mwaka 2014.

Mbunge huyo alitupwa jela na mkono wa sheria baada ya kukutwa na hatia ya kufanya vurugu na kumshambulia polisi katika uchaguzi wa kumtafuta Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Machi mwaka jana.

Mahakama hiyo pia ilimhukumu kifungo cha nje cha miezi sita, dereva wa Lijuakali, Stephano Mgata aliyekuwa akishtakiwa pamoja na mbunge huyo.

Muda mfupi baada ya Mahakama hiyo kutoa hukumu hiyo na Lijuakali kupelekwa gerezani chini ya ulinzi mkali kuanza kutumikia adhabu yake, Katibu wa Chadema mkoa wa Morogoro, Samuel Kitwika alisema kuwa hawakuridhishwa na uamuzi huo wa mahakama na kwamba wataka rufaa katika mahakama ya juu.

Naye Mbunge wa viti maalum mkoa wa Morogoro kwa tiketi ya Chadema, Devotha Minja alidai kuwa anaamini uamuzi huo ulitokana na shinikizo kutoka alikokuita ‘juu’ hivyo watakata rufaa.

Hata hivyo, wanasheria wameeleza kuwa Lijuakali hatapoteza sifa za kuwa mbunge wa jimbo la Kilombero kwani kifungo chake hakizidi miezi sita, kwa mujibu wa sheria.

Baada ya kutinga fainali, Azam yamtangaza Kocha Mpya Mromania
Trump aigeuka Urusi sakata la udukuzi wa mitandao, aipa 'za uso'