Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimeelezea mazingira ya kifo cha ghafla cha Mbunge wa zamani wa jimbo la Moshi Mjini (2000-2015), Phillemon Ndesamburo kilichotokea leo.

Katibu wa Chadema Mkoa wa Kilimanjaro, Bazil Lema amesema kuwa Ndesamburo maarufu kama Ndesapesa alifika katika ofisi za chama hicho kama ilivyo kawaida yake kufanya kazi, lakini ilipofika majira ya saa nne asubuhi aliugua ghafla.

Lema alisema kuwa Ndesamburo alikimbizwa katika hospitali ya rufaa ya KCMC lakini alifariki dunia wakati madaktari wakiendelea kumpatia huduma.

Kiongozi huyo wa Chadema aliongeza kuwa kutokana na mazingira hayo, mwili wa marehemu utachunguzwa ili kubaini chanzo cha kifo chake.

“Baada ya mwili kufanyiwa uchunguzi taarifa rasmi kuhusu kifo chake zitatolewa na uongozi wa chama pamoja na familia,” Lema anakaririwa na Mwananchi.

Marehemu ndesamburo alikuwa Mwenyekiti wa Chadema mkoa wa Kilimanjaro, pia mfadhiri mkubwa wa chama hicho.

Taarifa za kifo chake zilitolewa rasmi Bungeni na kiongozi wa kambi rasmi ya upinzani bungeni ambaye pia ni mwenyekiti wa Chadema-Taifa, Freeman Mbowe.

Taifa Stars Kufanya Mazoezi Usiku
Idris Sultan awapa ‘neno’ wanaopost iftari zao mitandaoni