Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Hashim Issa Juma amesema watamkaribisha Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif endapo chama chake kitakufa.

Juma amesema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari, ambapo amesema kuwa Chadema hawafurahishwi na kinachoendelea ndani ya CUF na endapo kitakufa wao watajiimarisha zaidi Zanzibar na kumpa nafasi Maalim kugombea Urais visiwani humo kupitia Chama hicho.

”Chadema na CUF ni kitu kimoja, kwa hiyo CUF kikitetereka sisi tutaimarika zaidi na kushika nguvu Zanzibar na sisi tutawakaribisha wagombea wote Zanzibar wachukue fomu na kugombea kupitia Chadema na hiyo ndio mipango yetu kama Baraza la Wazee,” amesema Hashim Issa.

Aidha amesisitiza kuwa sababu kuu ya msingi ya Chadema na CUF kuungana ilikuwa ni kukubalika kwa CUF kwa zaidi ya asilimia 80 katika visiwa vya Zanzibar lakini kwasasa Chama cha Mapinduzi (CCM) kikifanikiwa kuipangua CUF Zanzibar, Chadema haitashindwa kuchukua hatamu huko.

Hata hivyo, kwa upande mwingine Mwenyekiti huyo amesema wao kama Baraza la Wazee wataendelea kuhakikisha Chadema inaendelea kuimarika nchini kote hususani Zanzibar kwasababu wameona CUF inaweza kuvunjika kutokana na hali ilivyo sasa.

 

TCRA yainyooshea kidole mitandao inayorusha maudhui bila usajili
Bongo Star Search yarejea upya, Madam Rita atoa ombi Serikalini