Zikiwa zimebaki siku 3 zoezi la kupiga kura kumchagua rais wa Tanzania, wabunge na madiwani likamilike, Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimedai kuwa kimefanya tathmini na kugundua asilimia zitakazompa ushindi mgombea wake, Edward Lowassa.

Akiongea na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa kampeni wa chama hicho kinachoungwa mkono na vyama vya upinzani vinavyounda Ukawa, Reginald Munisi alisema kuwa tathimin hiyo imebaini kuwa Lowassa atashinda kwa asilimia 61 za kura zote.

“Wiki iliyopita tulifanya tathmini yetu. Kama ni chama cha siasa ni lazima ufanye jambo hili ili kuona utashinda kwa asilimia ngapi na unakubalika kwa kiasi gani. Tumebaini kuwa tutashinda kwa asilimia 61 na hata ikipungua haitazidi asilimia 58,” alisema.

Alisema kuwa tathmini hiyo iliwahusisha wapiga kura 30,000 waliofanyiwa utafiti katika mikoa mbalimbali.

Munisi aliele alieleza kuwa kutokana na hali hiyo, ndio sababu CCM wamekuwa wakijipanga kufanya hujuma mbalimbali alizodai kuwa zitahusisha Tanesco na mawasiliano husasan katika maeneo ambayo yanaaminika kuwa ni ngome ya chama hicho. Pia, alieleza kuwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeanza kuwatengenezea CCM bao la mkono kwa kuwa imekuwa ikipuuzia maombi yao ya kutaka kufanya marekebisho katika mapungufu ya msingi pamoja na kukagua mfumo mpya wa kuhesabia kura kwa njia ya kieletroniki.

Aidha, Munisi aliitaka Tume kuhakikisha inatenda haki ili kuepusha vurugu zinazoweza kujitokeza endapo taratibu na sheria hazitafuatwa katika mchakato mzima wa kupiga na kuhesabu kura.

Tathmini hiyo inatoa asilimia pungufu kulinganisha na ile iliyotajwa na mwenyekiti mwenza wa Ukawa, James Mbatia September 24, iliyodai kuwapa ushindi wa asilimia 71.

Hata hivyo, Munisi alieleza kuwa endapo watashindwa katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu na ikabainika kuwa taratibu na sheria zilifuatwa watakubali matokeo lakini sio vinginevyo.

 

FIFA Yamuingiza Kikaangoni Franz Beckenbauer
Magufuli: Hakuna Anaenidai…