Chama cha Demokrasia na Maendeleo kimesema kuwa hakijapokea barua yeyote kutoka bungeni ikiwataka kupeleka majina ya wagombea ubunge wa Afrika Mashariki (EALA).

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano, Owen Mwandumbya, amesema kuwa chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kinasubiri barua ya maelekezo kutoka bungeni lakini mpaka sasa hakijapokea.

Aidha, Uchaguzi wa wabunge wa EALA uliingia dosari baada ya wagombea wa Chadema, Lawrence Masha na Ezekiah Wenje kupigiwa kura za hapana hivyo kukosa wawakilishi wa nafasi ya ubunge wa Afrika Mashariki.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Itifaki, Mawasiliano, Uenezi na Mambo ya Nje wa Chadema, John Mrema amesema kuwa mpaka sasa hawajapata barua kutoka kwa katibu wa bunge Dkt. Thomas Kashililah kuhusu hatua wanazopaswa kuchukua.

“Tangu umalizike uchaguzi wa awali hatujapata taarifa zozote kutoka Ofisi ya Bunge, tunasubiri barua kutoka kwa Katibu wa Bunge mchakato gani ufanyike ili suala hilo lifikie muafaka,”amesema Mrema.

Hata hivyo, Spika wa Bunge, Job Ndugai amesema kuwa kama Chadema watapeleka wagombea waliokataliwa basi wategemee majibu yale yale na kwamba atalazimika kutumia utaratibu mwingine.

 

Wahariri Wamgeukia Profesa Lipumba Sakata la Uvamizi wa Mkutano
Magazeti ya Tanzania leo Aprili 27, 2017