Sakata la viongozi na wanachama wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kukihama chama hicho linazidi kuchukua sura mpya baada ya ngome ya chama hicho Iringa Mjini kuzidi kuyeyuka na huwenda kuzimika kabisa mithiri ya mshumaa kwenye pepo la ufukweni.

Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, Chama Cha Demokrasia na Maendeleo kiliibuka na ushindi wa Kata 14 kati ya Kata 18 zilizopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Iringa huku Chama Cha Mapinduzi (CCM) kikiambulia Kata 4.

Aidha, mpaka sasa upepo umebadilika ndani ya chama hicho mara baada ya kubakiwa na Kata 7 kati ya 14 ambazo kilishinda katika uchaguzi huo, baada ya madiwani wa Kata 7 kujiuzuru nyadhifa zao na kujiunga na CCM.

Viongozi hao wa Chadema wamedai moja ya sababu za kujiengua katika chama hicho ni kutokuridhishwa na utendaji wa chama hicho huku wakimtaja mbunge wa Iringa mjini, Mchungaji Peter Msigwa kwa kutumia ubabe na kutowasikiliza viongozi wenzake ndani ya chama hicho.

Moja ya madiwani hao ni Joseph Lyata aliyekuwa diwani wa Kata ya Kwakilosa kwa tiketi ya Chadema ambaye pia alikuwa mwenyekiti wa madiwani kanda ya Nyasa.
 
Lyata alishawahi kuwa naibu meya wa Manispaa ya Iringa kabla ya nafasi hiyo kuchukuliwa na Dady Igogo ambaye pia amejivua uanachama Chadema na kujiunga na Chama cha Mapinduzi (CCM).

Madiwani waliojiuzuru kutoka Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na kujiunga na CCM Manispaa ya Iringa Mjini ni pamoja na;

  1. Joseph Nzala Lyata – Kata ya Kwakilosa
  2. Oscar Kafuka – Kata ya Mkwawa
  3. Tandes Gabriel Sanga – Kata ya Ruaha
  4. Anjelus Mbongo Lijuja – Kata ya Mwangata
  5. Dadi Johansen Igogo – ambaye alikuwa Naibu Meya wa Manispaa ya Iringa- Kata ya Gangilonga
  6. Edgar Mgimwa- ambaye alikuwa Kata ya Kihesa na kuhamia CCM ambaye kwasasa anaiongoza Kata kwa tiketi ya CCM.
  7. Baraka  Jeremiah Kimata – Ambaye kwa sasa ni diwani kupitia CCM.

Pamoja na Lugano Mwanyingi, Leah Charles Mleleu na Hasna Daudi Mwangazi wa Viti Maalum.

Magazeti ya ndani na nje ya Tanzania leo Februari 22, 2018
Video: Tunashirikiana vizuri na wapinzani Ubungo- DC Kisare