Rapa Chid Benz ambaye takribani mwezi mmoja uliopita alisaidiwa na uongozi wa Tip Top Connection kuwekwa katika kituo maalum cha kusaidia waathirika wa dawa za kulevya (Sober House) kilichoko Bagamoyo mkoa wa Pwani ameripotiwa kurotoka katika kituo hicho.

Meneja wa kituo hicho, Tumaini Majura amethibitisha tukio hilo akieleza kuwa Chid Benz alianza kuonesha nia ya kuondoka katika kituo hicho kabla ya muda wake wa matibabu kukamilika na kwamba ingawa walimsihi sana, aliweza kufanikisha nia yake.

“Ni siku 28 tu alikaa, lakini alitakiwa kukaa kwa muda wa angalau miezi mitatu ili kurudi katika hali yake ya kawaida,” Majura alisema katika mahojiano na Global Publishers.

“Nafikiri ni uamuzi wake binafsi maana siku moja meneja wake (Babu Tale) alikuja kumjulia hali, alipotaka kuondoka aling’ang’ania kuondoka naye. Sisi pamoja na Tale tulimsihi sana kubaki lakini alikataa,” aliongeza.

Chid Benz alipelekwa katika nyumba hiyo kwa msaada wa Meneja wa Tip Top, Babu Tale baad aya kuomba hadharani kusaidiwa ili aachane na dawa za kulevya zilizokuwa zimemletea madhara makubwa ikiwa ni pamoja na kudhoofu mwili kwa kiwango kikubwa.

Alipotafutwa kuzungumzia suala hilo na mtandao huo alikataa kuzungumza na kueleza kuwa mambo yake yote aulizwe Babu Tale.

Kitambi Aelezea Kilichoitafuna Azam FC Dhidi Ya Young Africans
Ronald Koeman Kusaini Mkataba Mpya Kwa Masharti