Rais wa China, Xi Jinping amesema kuwa nchi hiyo itatoa jumla ya dola bilioni 60 za Marekani kwenye mpango wake wa miaka mitatu ya ushirikiano na Afrika katika shughuli za maendeleo.

Ameyasema hayo wakati akifungua Mkutano wa Jukwaa la Ushirikiano kati ya China na Afrika (FOCAC) unaofanyika jijini Beijing nchini China.

Rais Xi Jinping ameahidi kuwa nchi yake itatoa ushirikiano ili kuhakikisha kwamba amani ya kudumu inapatikana Barani Afrika, hatua ambayo ni muhimu kwa ustawi wa nchi za Afrika.

Aidha, maeneo mengine ambayo Rais huyo ameahidi kulisaidia Bara la Afrika ni pamoja na ujenzi wa miundombinu, ushirikiano katika sekta ya biashara na huduma za afya.

Mkutano huo ulianza kwa sherehe ya ukaribisho na baadae viongozi kutoka nchi mbalimbali barani Afrika na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres walipata fursa ya kupiga picha ya pamoja na mwenyeji wao Rais wa China.

Hata hivyo, mwakilishi kutoka Tanzania ambaye ni Waziri Mkuu, Kasim Majaliwa ambaye anamwakilisha Rais Dkt. John Magufuli katika mkutano huo alisalimiana na Rais Jinping baada ya ufunguzi.

Video: JPM awapa tano wabunge CCM, awapiga dongo upinzani
IGP Sirro afanya mabadiliko ya Makamanda wa Polisi wa Mikoa