Rais wa Ghana, Nana Akufo – Addo ametangaza kuwa serikali yake itawalipia bili za maji wananchi kwa muda wa miezi mitatu kufuatia harakati za nchi hiyo za kupambana na virusi vya Covid 19.

Nchi ya Ghana imethibitisha visa 214 vya wagonjwa wa virusi vya corona na imepoteza watu watano kutokana na ugonjwa huo.

Wiki iliyopita, baadhi ya maeneo nchini humo wakazi wake walianza karantini ya kutotoka nje ambapo mji wa Accra, Tema na Kumasi ndiyo iliyohusika kwani ilionekana kuwa na kiwango kikubwa cha maambukizi.

Kupitia hotuba yake kwa wanachi iliyoonyeshwa kwenye runinga, Rais Akufo-Addo amesema , wahudumu wote wa afya wanaohudumia wagonjwa wa covid -19 watapata nyongeza za mishahara na hawatalipa kodi yeyote kwa muda wa miezi mitatu.

Ikumbukwe kuwa hivi karibuni Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) limesema janga la virusi vya Corona limelemaza uchumi wa dunia na litasababisha mdororo mkubwa wa uchumi wenye athari mbaya kushinda mzozo wa kifedha wa mwaka 2008.

Waziri wa Afya ashushwa cheo kwa kuipeleka familia baharini
Corona Tanzania: Idadi ya waliopona yaongezeka