Waliokua wachezaji wa Arsenal ya England Alex Song na Johan Djourou ni miongoni mwa wachezaji waliofukuzwa kwenye klabu ya FC Sion, baada ya ligi ya Uswiz kusimamishwa, kufuatia janga la kusambaa kwa Virusi vya Corona.

Wachezaji wengine waliotimuliwa klabuni hapo ni nahodha Xavier Kouassi, kiungo wa zamani wa Fulham Pajtim Kasami, Ermir Lenjani, Seydou Doumbia, Mickael Facchinetti, Christian Zock na Birama Ndoy

Maamuzi ya kutimuliwa kwa wachezaji hao, yamekuja baada ya kukataa kusaini mkataba wa kukatwa mshahara katika kipindi hiki ambacho ligi kuu ya Uswiz imesimama.

Ligi ya Uswiz ilisimamishwa rasmi Machi Mosi, baada ya serikali ya nchi hiyo kutoa tangazo la kusimamisha shughuli za mikusanyiko ya watu, kwa kuhofia maambukizi ya virusi vya Corona.

FC Sion ni miongoni mwa timu shiriki katika ligi kuu ya Uswiz, na ipo katika nafasi mbaya ya kushuka daraja, kufuatia tofauti ya alama nne dhidi ya timu zilizo kwenye hatari hiyo.

Klabu hiyo imesaliwa na michezo 13 kabla ya kufikia tamati kwa msimu huu wa 2019/20.

Serikali yaanzisha kitengo cha usimamizi wa majengo
Zimbabwe yathibitisha kisa cha kwanza mgonjwa wa Corona