Mabingwa wa soka barani Ulaya klabu ya Real Madrid imefanikiwa kumsajili mlinda mlango kutoka nchini Ubelgiji Thibaut Courtois akitokea Chelsea ya nchini England.

Real Madrid wamekamilisha dili hilo kwa kutoa kiasi cha pesa sambamba na kiungo wao kutoka nchini Croatia Mateo Kovacic, ambaye amejiunga na Chelsea kwa mkopo hadi mwishoni mwa msimu wa 2018/19.

Courtois, mwenye umri wa miaka 26, alikua anahusishwa na mpango wa kujiunga na wababe hao wa Santiago Bernabeu tangu aliporejea kutoka kwenye majukumu ya kuitumikia timu yake ya taifa kwenye fainali za kombe la dunia zilizofanyika nchini Urusi.

Mpango huo uliibuliwa na Real Madrid huku mkataba wa mlinda mlango huyo na klabu ya Chelsea ukitarajiwa kufikia kikomo mwishoni mwa msimu wa 2018/19, na tayari alikua ameshakataa kusaini mkataba mpya kwa shinikizo la kutaka kuondoka jijini London.

“Usiku huu (Jana) tumefikia makubaliano na uongozi wa klabu ya Chelsea kuhusu usajili wa Thibaut Courtois, tunathibitisha kumsajili mlinda mlango huyu, tumekubalia kumpeleka kwa mkopo Mateo Kovacic kwa mkopo kwa wenzetu wa jijini London.” Imeeleza taarifa iliyoandikwa kwenye ukurasa wa Twitter wa klabu ya Real Madrid.

Hata hivyo pesa iliyotumika kusajiliwa kwa Courtois haijawekwa wazi, kufuatia makubaliano yaliyofikiwa na pande hizo mbili.

Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Agosti 9, 2018
Tanzia: Mzee Majuto afariki dunia