Terrence Crawford amefanikiwa kutetea mkanda wake wa ubingwa wa dunia wa Masumbwi wa WBO muda mfupi uliopita baada ya kumshinda kwa KO, Amir Khan kwa namna iliyoacha gumzo.

Pambano hilo limeshuhudiwa katika ukumbi wa Madison Square Garden, jijini New York nchini Marekani.

Crawford ambaye alikuwa ameonesha kulitawala pambano hilo tangu raundi ya kwanza akimdondosha Khan, alicheza ‘faulu’ nzito kwenye raundi ya sita akishusha konde zito kwenye eneo la nyeti za mpinzani wake hali iliyozua sintofahamu.

Konde hilo lilimsababishia maumivu makali Khan ambaye baada ya kusaidiwa kwa muda, daktari wa kona yake alimpa ishara daktari wa ulingoni kuwa hawezi tena kuendelea na pambano.

Ingawa mwamuzi alikuwa amemuonya mara mbili Crawford kwa kurusha makonde chini ya kitovu (low blow), amelazimika kumpa ushindi kwa namna hiyo, hali iliyozua mjadala kwa mashabiki kama faulu inaweza kumsaidia mchezaji kushinda kwa KO.

Crawford alikuwa amepewa nafasi zaidi ya kushinda pambano hilo tangu awali kutokana na uwezo wake, umri wake pamoja na rekodi yake akitajwa kama bondia namba mbili kwa ubora duniani kwa mujibu wa The Rings.

Bingwa wa zamani wa masumbwi ya uzito wa juu, Linox Lewis ambaye ni Muingereza alisema kabla ya kuanza pambano hilo kuwa moyo wake uko na Khan ambaye ni muingereza mwenzake lakini akili yake inamwambia mshindi ni Crawford.


Mashabiki wa Khan wametaka Crawford asipewe ushindi huo kwa jinsi ambavyo amecheza faulu ya wazi na nzito dhidi ya bondia wao.

Picha: Mabegi, magunia ya pesa yaliyokutwa nyumbani kwa al-Bashir yawekwa wazi
Bodi ya Filamu yalaani vikali kauli ya Musukuma