Mshambuliaji mpya wa mabingwa wa soka nchini Italia, Juventus FC, Cristiano Ronaldo huenda akaonekana kwa mara ya kwanza akiwa na jezi ya klabu hiyo uwanjani, wakati wa mchezo wa kirafiki dhidi ya waliokua waajiri wake Real Madrid.

Ronaldo anapewa nafasi kubwa ya kucheza mchezo huo utakaochezwa kesho Jumamosi, baada ya kuonekana katika maozezi ya pamoja na kikosi cha Juventus.

Mshambuliaji huyo alianza mazoezi ya pamoja na wachezaji wenzake mapema juma hili baada ya kikosi cha Juve kurejea nchini Italia kikitokea Marekani kilipokua kimekwenda kwa ajili ya michezo kadhaa ya kirafiki, kupitia michuano ya Kombe La Mabingwa wa Kimataifa (ICC).

Mbali na kupewa matarajio ya kucheza dhidi ya Real Madrid ambapo ataishambulia ngome ya waajiri wake wa zamani, Ronaldo ana uhakika wa kucheza mchezo wa kwanza wa ligi ambao utashuhudia kikosi cha Massimiliano Allegri kikianza kampeni ya kutetea taji la Italia, kwa kupapatuana na Chievo, Agosti 18.

Ronaldo alijiunga na mabingwa hao wa Italia mwezi uliopita kwa ada ya Euro milioni 100 akitokea Real Madrid alipocheza kwa mafanikio makubwa tangu mwaka 2009.

Akiwa mjini Madrid, mshambuliaji huyo ambaye pia ni nahodha wa timu ya taifa ya Ureno alifanikiwa kucheza michezo 292 na kufunga mabao 311, huku akitwaa mataji manne wa Ligi ya Mabingwa Barani Ulaya (UEFA Champions League: 2013–14, 2015–16, 2016–17, 2017–18).

Upande wa ligi, Ronaldo ametwaa taji la La Liga mara mbili (2011–12, 2016–17), Kombe la mfalme (Copa del Rey mara mbili: 2010–11, 2013–14), kombe la Hispania (Supercopa de España: 2012, 2017), taji la UEFA Super Cup 2014, 2017 na taji la Klabu Bingwa Duniani (FIFA Club World Cup: 2014, 2016, 2017).

Ousmane Dembele atua London, akutana na wachezaji wa Arsenal
Mambo ya kufanya ili kuongezwa mshahara na mwajiri wako