Familia ya mfanyabiashara maarufu nchini, Mohammed Dewji ‘Mo’ imetangaza dau la Shilingi bilioni 1 za Kitanzania kwa mtu yeyote atakayewezesha kupatikana kwa bilionea huyo.

Akizungumza kwa niaba ya familia mbele ya waandishi wa habari, Azim Dewji amesema yeyote atakayetoa taarifa zitakuwa za siri huku akiwaomba Watanzania kuendelea kuwaombea familia hiyo na mtoto wao apatikane akiwa salama.

“Yeyote atakayewezesha kupatikana kwa mtoto wetu mpendwa Mohammed atazawadiwa Sh1 bilioni.” amesema Azim, ambaye amejitambulikuwa kuwa ni mwanafamilia.

Katika mkutano huo wa leo Jumatatu uliohudhuriwa na vyombo vya habari vya ndani na nje ya nchi, baba mzazi wa ‘Mo’,  Gullam Hussein alikuwa amekaa pembeni mwa Azim wakati akisoma taarifa hiyo ya familia.

Azim amesema yeyote mwenye taarifa anaweza kuwasiliana nao kwa namba 0755030014 au 0717208478 na 0784783228.

Mo anayekadiriwa kuwa na utajiri wa Shilingi Trilioni 3.5 alitekwa Alhamisi iliyopita katika Hoteli ya Collosseum jijini Dar es Salaam alipokwenda kufanya mazoezi saa 11 alfajiri.

Mo ni mwekezaji wa klabu ya Simba na alikuwa katika mchakato wa kuwekeza Shilingi bilioni 20 ili amiliki hisa 49 za klabu hiyo ya Msimbazi.

Aliyemtwanga McGregor ataka kuzichapa na Mayweather
Atakayempata Mo Dewji kupewa Sh1 bilioni