Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Daniel Chongolo amezindua zoezi la uandikishaji wa vitambulisho vya Taifa kwa watu wenye ulemavu ili kuwarahisishia kupata huduma hiyo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo leo Septemba 12, katika viwanja vya Shule ya msingi Makurumla iliyopo kata ya Ndugumbi wilaya ya Kinondoni  jijini Dar es salaam, amesema mpaka sasa asilimia 60 ya wananchi wameshaandikishwa ili kupata vitambulisho vya taifa.

“Kumekuwa na changamoto kwa watu wenye ulemavu katika kujiandikisha usajili wa vitambulisho vya Taifa hasa  pale unapokuta walemavu wamekaa sehemu moja na watu wasio na ulemavu,sasa ni wakati wao kupata urahisi wa zoezi hili kwa hizi siku tatu,” amesema DC Chongolo.

Amesema kuwa kujisajili kwenye Vitambulisho vya Taifa kwa walemavu kutasaidia kujua aina ya ulemavu walionao na kujua sehemu wanayotokea na hii itarahisisha kuwapata.

Kwa upande wake Afisa Msajili wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Wilaya ya Kinondoni, Dicksoni Mbanga amesema wanategemea kuwafikia Walemavu wengi katika wilaya ya  kinondoni na zoezi hilo litafanyikia katika vituo vilivyopo wilayani hapo.

 

JPM atoa maagizo mazito
Chadema kutafakari kumpa Maalim Seif kuwania Urais