Mkuu wa Wilaya ya Wanging’ombe Mkoani Njombe, Ally Kassinge ametoa wiki mbili kwa Seminari ya Kidugala iliyopo chini ya Kanisa la Kiinjili na Kilutheri KKKT kukaa na Mkurugenzi wa halmashauri hiyo kutengeneza makubaliano ya kisheria yatakayosaidia wananchi kumiliki shule ya msingi kidugala itakayojengwa na seminari hiyo.

Ametoa agizo hilo mara baada ya kufanya ziara kijijini hapo kwa ajili ya kusuruhisha mgogoro wa mipaka kati ya Seminari hiyo na wananchi wa kijiji hicho uliodumu takribani miaka 20 hali iliyopelekea wanafunzi kusoma katika shule yenye uchakavu wa Majengo.

‘’Mgogoro huu ni wa muda mrefu na ulibeba hisia za wananchi hasa wakiangalia namna ambavyo watoto wao wanasoma katika majengo yaliyochakaa yenye nyufa, awali kanisa lilitaka lijenge kwa asilimia 80 na kuwataka nyinyi wananchi mchangie kwa asilimia 20 hapo ndo mvutano ulipokuja, niwaambie sasa kanisa limekubali kujenga kwa asilimia 100,’’amesema DC Kassinge.

Amesema kuwa makubaliano kati ya mkurugenzi na kanisa pamoja na kijiji yaende sambamba na mpango kazi ambao utaonyesha ramani ya majengo ya serikali jinsi yanavyotakiwa kuwa.

Kwa upande wa mkurugenzi wa halmashauri wa Mji wa Wanging’ombe, Amina Kiwanuka amesema kuwa mgogoro huo umekuwa ukikwamisha jitihadi za halmashauri yake kukarabati shule hiyo.

Hata hivyo, Mkuu wa Seminari ya Kidugala mchungaji, Award  Lyawene amesema kuwa kanisa limekubali kujenga shule hiyo katika kiwanja kingine chenye zaidi ya hekari 20 na kuweka miundombinu yote kwa asilimia 100 sio kama awali ambapo waliwatakiwa wananchi kuchangia kwa silimia 20.

Tanzania yapanda nafasi 9 viwango vya FIFA
Serikali kuimarisha ulinzi baharini