Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Ruth Msafiri ameapa kupambana na kiongozi yeyote atakayediriki kumchangisha mzazi fedha ya dawati kama walivyochangishwa baadhi ya wazazi katika shule ya Sekondari Maheve pamoja na shule ya Sekondari Mabati zilizopo katika halmashauri ya mji wa Njombe.

Ameyasema hayo mjini Njombe alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, ambapo amesema kuwa utaratibu wa kufuata waraka wa elimu bure uko pale pale, hivyo suala la kumchangisha mzazi dawati ni kinyume na maagizo ya serikali.

“Nimeshaagiza kwa mkurugenzi, waratibu elimu wa kata waliofanya hayo wachukuliwe hatua na hatua ya kwanza ni kumpunguzia madaraka sio wahamishwe hatutaki kuhamisha matatizo, nimesema waondolewe madaraka yao waratibu elimu walioandika barua ambazo ninazo mimi za kutoa maelekezo yaliyo kinyume ya kuwachangisha wazazi lakini na wakuu wa shule waliyoyatekeleza hayo na wenyewe waondolewe ili liwe fundisho kwa wengine,”amesema DC Msafiri

Aidha, DC Msafiri amewaagiza wakurugenzi wote wa halmashauri tatu za wilaya ya Njombe kupita katika kata zote 37 ili kuthibitisha kama hakuna mzazi aliyeombwa wala kulazimishwa kutoa mchango kwa ajili ya miundombinu ya shule.

Hata hivyo, siku za hivi karibuni, mkuu huyo wa wilaya aliagiza kushushwa vyeo afisa elimu kata ya Ramadhani, Estar Mjululu, na Huruma Mgeyekwa pamoja na Mkuu wa Shule ya Sekondari Maheve, Valeno Kitalika kwa makosa ya kuwatoza wazazi michango, huku diwani wa kata hiyo George Menson Sanga akipinga maamuzi hayo.

Uganda: DJ auawa kwa kucheza muziki mbaya
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Januari 19, 2019