Viongozi wa Jeshi la Magerera wameridhia kuwaachia wananchi eneo la Ardhi lenye ukubwa wa Ekari 6.2 katika mtaa wa Mtepwezi Manispaa ya Mtwara Mikindani, lililokuwa na mgogoro kwa zaidi ya miaka kumi.

Maamuzi ya Viongozi hao wa Jeshi la Magereza yamekuja kufuatia mapendekezo ya Mkuu wa wilaya ya Mtwara, Evod Mmanda aliyefanya mkutano katika eneo hilo Februari mbili mwaka huu wa 2019 katika eneo hilo ambalo lilidaiwa kuwa na mgogoro uliodumu tangu mwaka 2006  na kukutanisha pande zote mbili zinazozozana kati ya wananchi na Magereza.

Miongoni mwa wahanga wa mgogoro huo wamesema kuwa miaka yote walikua wakiishi na kuendesha shughuli zao katika eneo hilo lakini kilicho washangaza ni baada ya Maafisa kutoka Jeshi la Magereza kupita katika maeneo yao na kuweka mipaka bila kuwashirikisha sambamba na kuharibu baadhi ya mali ikiwemo mazao na kubomoa Nyumba.

“Nimeamua kuja mwenyewe nataka kuona eneo ambalo mmeleta malalamiko ofisini, na nitahitaji kupata pia maelezo kutoka kwa wajumbe wa ile kamati mlioleta malalamiko yenu …. Nasra wewe ulikua miongoni mwa wale wajumbe niambie historia ya hapa na maelezo yote mmayo yajua,”amesema Mmanda

Aidha, wananchi hao wamesema kuwa walishafikisha malalamiko yao kwa viongozi mbalimbali wakiwemo wakuu wa wilaya wa awamu mbili zilizopita pamoja na mkuu wa mkoa aliyepita na viongozi hao walishafika katika eneo hilo la mgogoro lakini mpaka siku hiyo ya mkutano hakukuwa na ufumbuzi wa Mgogoro huo.

Kwa upande wa Jeshi la Magereza kupitia Kaimu mkuu wa Magereza wa mkoa huo, ACP Isaack Kangura amesema kuwa meneo ya majeshi mipaka yake inafahamika lakini kilichofanyika katika eneo hilo ni ujirani mwema wa kuwaachia wananchi kulima kwa muda lakini shida inatokea baada ya kuwa wabishi unapofika muda wa kutakiwa kuondoka.

Hata hivyo, baada ya kusikiliza maelezo ya pande zote mbili mkuu huyo wa wilaya ameagiza kuundwa kwa tume itakayojumuisha wawakilishi kutoka pande zote, Magereza, Wawakilishi wa wananchi akiwemo Afisa Mtendaji wa Mtaa huo pamoja na Maafisa Ardhi kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani na kuagiza kupima eneo la Ekari 6.2 kutoka katika eneo hilo na kuwakabidhi wananchi kisha Jeshi nao kuweka mipaka ya uhakika katika eneo litakalo baki.

Video: Mfungwa Aliyesamehewa na Magufuli akutwa na sare za Jeshi
Video: Bunge laibua ubadhirifu wa Sh31 bilioni za umma, Miradi saba bomu NSSF