Mvutano kati ya Rais wa Marekani, Donald Trump na viongozi wa chama cha Democratic kuhusu ujenzi wa ukuta wa mpakani unaotakiwa na rais huyo, umeingia sura mpya baada ya Trump kuondoka kwa hasira kwenye mazungumzo.

Tofauti kuhusu ukuta huo kwenye mpaka kati ya Marekani na Mexico, ambao umekataliwa na wanachama wa chama cha Democrats, umesababisha kufungwa kwa baadhi ya wizara na Idara kadhaa za serikali kwa muda wa siku kumi na tisa sasa.

Katika mkutano huo baina ya Rais Trump na viongozi wa chama cha Democratic bungeni, Nancy Pelosi ambaye ni spika wa baraza la wawakilishi na Chuck Schumer, kiongozi wa wanachama wa Democrats katika baraza la seneti, haukudumu kwa muda mrefu.

Aidha, mazungumzo baina yao yalikuwa yakijaribu kwa mara nyingine kutafuta muafaka wa kumaliza mkwamo wa shughuli za serikali, ulioanza siku 19 zilizopita baada ya Trump kukataa kusaini mpango wa bajeti ambao haujumuishi dola bilioni 5.7 anazozitaka kwa ajili ya ujenzi wa ukuta katika mpaka baina ya Marekani na Mexico, ambao ni ahadi yake kuu ya kampeni yake ya urais.

Hata hivyo, katika ukurasa wake wa Twitter, Trump ameandika kuwa ”Nimeondoka sasa hivi katika mkutano na Chuck na Nancy, ambao ulikuwa ni kupoteza muda kabisa. nimewauliza ikiwa nitazifungua haraka shughuli za serikali, kipi kitafanyika katika siku 30 zitakazofuata, mtaridhia fedha za kujenga ukuta mpakani, Nancy akajibu ‘hapana’, nikawaambia, ‘kwa heri, hakuna kitakachofanyika hapa’

Serikali yazinyooshea kidole shule binafsi
Muungano wa Vyama vya Upinzani Congo DR wayakataa matokeo