Dereva wa bilionea Mohamed Dewji ambaye ametekwa na watu wasiojulikana, ameeleza jinsi ambavyo Bosi wake huyo alivyokuwa anaishi.

Akizungumza leo kupitia Clouds Fm, dereva huyo amesema kuwa ni jambo la kawaida kwa mfanyabiashara huyo tajiri kuendesha gari lake mwenyewe kwani alikuwa anaamini ana amani.

“Mo Dewji ni tajiri lakini anaishi maisha fulani hivi kama vile sio tajiri. Yaani alikuwa hana hofu na raia kwa sababu yeye kila mtu anayekutana naye ni kama vile anajuana naye miaka mingi,” alisema.

Dereva huyo ambaye amefanya kazi kwa Mo tangu mwaka 2001 ameeleza kuwa Mo alikuwa anajiamini na hakuwa na uoga dhidi ya raia, lakini aliwahi kumtahadharisha mwaka huu kuwa amekuwa akipokea jumbe za vitisho.

“Kuna kipindi aliniambia, ‘bwana kwa huku tunakoenda inabidi kuwa makini’. Nikamuuliza kwanini, akasema kuna kipindi alikuwa anapata meseji halafu kama za vitisho-vitisho. Ilikuwa kama miezi minne iliyopita,” aliongeza.

Kwa mujibu wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Mo alitekwa na watu wasiojulikana mapema leo asubuhi katika hoteli ya Colleseum jijini Dar es Salaam.

Polisi wanaendelea na msako na tayari wameshawakamata watu kadhaa wakihusishwa na tukio hilo.

Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Oktoba 12, 2018
RC Wangabo awatahadharisha Wakurugenzi na Madiwani