Mwaka 2021 unaelekea ukingoni, zikiwa zimesalia wiki tatu pekee kuuanza mwaka mpya 2022.

Kwa kipindi cha miezi 12 ya mwaka 2021, Tasnia ya muziki wa kizazi kipya imeonekana kuchangamka kwa kiwango kikubwa huku ushindani baina ya wasanii ukiongezeka na kutengeneza chachu ya wasanii mbali mbali kuwekeza nguvu kubwa katika kuhakikisha wanatoa nyimbo zenye kuweza kukidhi mahitaji ya mashabiki wa mziki huo ndani na hata nje ya mipaka ya Tanzania.

Licha ya ushindani huo mkubwa kushamiri kwenye muziki, wapo wasanii waliofanikiwa kujiandikia historia zao za kipekee, kutokana na mafanikio ya jitihada zao kwenye muziki, kwa kupata fursa mbali mbali ikiwamo kutajwa kwenye vinyang’anyiro vya tuzo mbali mbali za kimataifa, kutengeneza connections, kolabo kubwa, deals za Ubalozi wa makampuni makubwa (Indorsements)  nk.

Pamoja na mengi mazuri yaliyojiri ndani ya mwaka 2021, kundi kubwa la wasanii halitokisahau kipindi kigumu cha mpito wakati ambao Dunia ilikugubikwa na wimbi la kuenea kwa Virusi vya ugonjwa wa ‘Covid19’, kipindi ambacho kiziteteresha tasnia nyingi ikiwamo tasnia ya muziki. Kutokana na wasanii kukosa kufanya matamasha, yaliyolazimika kusimama kwa muda kupisha wimbi hilo.

Kwa zaidi ya kipindi cha zaidi ya mwaka mmoja wa kasi ya kuenea kwa ‘Covid-19’ wasanii wengi walijikita zaidi katika matumizi ya njia mbadala ili kujiingizia kipato, baadhi wenye biashara ya tofauti na muziki walijikita zaidi huko.

Na wakati huo huo sehemu pekee iliyokuwa kimbilio kubwa la wasanii wengi ni kwenye Digital Platforms, sehemu za kusikiliza na kupakuwa muziki kwa njia ya mtandao, ambayo ni moja ya njia zenye kuwaneemesha wasanii wengi kutokana na urahisi wake kwa kutengeneza pesa kwa wasanii.

Kupitia njia hizo wapo wasanii waliofanikiwa zaidi kiasi cha kusahau hata kutetereka kwa kiwanda cha muziki kutokana na janga la Covid-19, hii ni kulingana na namna walivyopigania kutoa kazi nzuri na rafiki kwa mashabiki wao, kiasi cha kuzifanya nyimbo zao kupata nafasi ya kusikilizwa zaidi kupitia Digital platform kama Apple Music, BoomPlay, Deezer, Spotify, Youtube nk.

Kuelekea kuufunga mwaka mtandao maarufu wa Kusikiliza na kupakuwa muziki mtandaoni ‘Boomplay’ umetoa orodha ya wasanii walioweza kuweka rekodi za kipekee kwa kufanya vizuri zaidi kwenye mtandao huo kwa mwaka 2021.

Kupitia ukurasa maalum wa mtandao wao wa Instagram Boomplay wameiweka wazi orodha hiyo iliyogawanyika katika vipengele visivyopungua 9, ambavyo ni :-

Wasanii wa Kiume walioongoza kwa mwaka 2021
   1: Rayvanny
   2: Mbosso
   3: AliKiba

Wasanii wa Kike walioongoza mwaka 2021
   1: Zuchu
   2: Nandy
   3: Anjella

Wasanii Chipukizi walioongoza mwaka 2021
     1: Mac Voice
     2: Jay Melody
     3: Rapcha

Wasanii waliotafutwa zaidi kwa mwaka 2021
  1: Diamond Platnumz
  2: Harmonize
  3: Rayvanny

Makundi yaliyoongoza kwa mwaka 2021
  1: Mabantu
  2: Rostam
  3: Weusi

Nyimbo zilizoongoza kusikilizwa kwa mwaka 2021
  1: Sukari by Zuchu
  2: For You by Marioo
  3: Baikoko by Mbosso ft DiamondPlatnumz

Nyimbo zilizoongozq kupendwa kwa mwaka 2021
  1: Sukari by Zuchu.
  2: Number One by Rayvanny ft Zuchu
  3: Baikoko by Mbosso ft DiamondPlatnumz

Nyimbo zilizofikisha streams Milioni 1 kwa haraka zaidi.
  1: Naanzaje by DiamondPlatnumz
  2: Sukari by Zuchu
  3: Nenda by Mac Voice

Kolabo za Kimataifa zilizoongoza kusikilizwa.
  1: IYO by DiamondPlatnumz ft Facolistic & Mapara  A Jazz
  2: Beer Tamu by Marioo ft Tyle ICU, Abbah & Visca
  3: Salute by Ali Kiba ft RudeBoy

Kutolewa kwa orodha hiyo kumeonyesha  taswira halisi ya namna amabavyo wasanii wamefanikiwa kujitengenezea nafasi zao kwa kuzitumia fursa za mitandao mbali mbali kujiingizia kipato.

Mpangilio wa Orodha hiyo pia umeibua mjadala baina ya wadau wa muziki, hoja kubwa ikiwa ni uhitaji wa uwapo wa tuzo za muziki nchini, kwa ajili ya wasanii ili kuwapa hamasa ya kuendelea kujituma na kufanya vizuri zaidi.

Nick Cannon amwaga machozi kifo cha mtoto wake mchanga
DC Longido atoa maagizo katika halmashauri