Dj wa Clouds Fm, DJ D Ommy ambaye hivi karibuni alizindua kwa vitendo mradi wake wa kuwakutanisha kwenye ngoma moja wasanii kadhaa, amefunguka jinsi alivyounganisha wakali wa RnB halisi (Jux na Ben Pol) na mkali wa ‘melodi’ za Bongo Fleva, Baraka Da Prince kwenye ngoma yake ‘DJ’.

Akizungumza na Dar24, DJ D Ommy amesema kuwa aliamua kuwakutanisha wakali hao kwenye ‘DJ’ na kuwapa wazo la kufanya wimbo huo, kutokana na hisia za muziki fulani uliokuwa unakuja kichwani kwake lakini bado haujafanyika.

Alisema kuwa baada ya kuwakutanisha wakali hao aliwapa wazo na mdundo ambao waliufanyia kazi usiku mmoja huku akisimamia hatua zote ili kupata ile ladha ambayo alikuwa anahisi itawafaa mashabiki wake.

“Unajua lengo la projects zangu ni kuwafanya mashabiki wangu wapate ladha ya muziki ninayohisi inatakiwa kuwepo lakini haipo kutokana na sababu mbalimbali. Kwahiyo ‘DJ’ ni moja kati ya miziki itakayotokana na hisia zangu za muziki na husimamia utayarishaji wake,” DJ D Ommy aliiambia Dar24.

Katika hatua nyingine, DJ huyo ambaye ni mshindi wa tuzo ya DJ Bora wa Afrika alisema kuwa tayari ameshakamilisha nyimbo zaidi ya 12 na kati ya hizo ni pamoja na Bongo-Marekani kolabo.

“Kuna ngoma nimefanikisha kolabo kati na wasanii wa Marekani na wasanii wetu wa Bongo. Itakuwa project kali sana na ya aina yake. Sitaki kuweka kila kitu wazi sasa, lakini tusubiri muda utafika,” DJ D Ommy aliiambia Dar24.

DJ huyo amepata mapokezi makubwa nchini Marekani ambapo mixing zake zinasikika kwenye moja kati ya radio zinazorusha matangazo yake kwa lugha ya Kiswahili, huku akipewa nafasi kwenye baadhi ya club za usiku kwenye majiji makubwa nchini humo.

Bofya hapa kusikiliza na kupakua wimbo wa DJ D Ommy feat. Jux, Barakah Da Prince na Ben Pol

Mkurugenzi UNDP atimuliwa nchini
Ujauzito Wamponza Serena Williams