Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe amewaambia wachezaji wa timu ya mpira wa miguu ya Tanzania Bara, ‘Kilimanjaro Stars’, kuwa Tanzania inahitaji ushindi katika michuano ya Kombe la Baraza la Soka la Afrika Mashariki (CECAFA).

Dk. Mwakyembe aliyesema hayo jana Novemba 29, usiku wakati wa hafla ya chakula cha jioni ambako alitumia baraza hilo kuwaaga vijana hao akiwataka wachezaji wa timu hiyo kwenda Kenya kujitahidi.

“Msidharau mechi,” amesema Dk. Mwakyembe huku akisisitiza: “Tunataka ushindi. Mnakwenda Kenya kwa niaba ya Watanzania. Najua mmejiandaa vizuri kwa mazoezi maana siku hizi huwezi kushinda kwa kumtegemea (kuroga). Siku hizi mazoezi ni basic component.

Akasisitiza: “Nina matumaini makubwa nanyi. Nendeni na baraka zangu tele na kila anayekuja mbele yenu ni kumtandika tu. Tandika wote. KIla anayekuja piga tu maana mna kila kitu.”

“Mkifanikiwa kuwatandika na kuingia nusu fainali itabidi niwashe gari tu na kuja kuwapa sapoti Kenya. Nitamwambia bwana mkubwa, wizara hii ina naibu waziri ambaye nitamwachia ofisi ili nije,” amesema.

Kwa upande wake, Kocha Mkuu wa timu hiyo, Ammy Ninje alimhakikishia Waziri Dk. Mwakyembe pamoja na Rais wa TFF, Wallace Karia kwamba kikosi hicho kimeunganishwa vema katika siku tatu walizokaa kambini.

Nahodha Msaidizi wa timu hiyo, Erasto Nyoni alishukuru kwa niaba ya wachezaji na timu hiyo kabla ya kuondoka leo saa 7.15 mchana kwenda Kenya kwa ndege ya Shirika la Ndege la Kenya (KQ).

Wachezaji watakaokuwako huko Kenya ni makipa Ramadhani Kabwili (Young Africans, Aishi Manula (Simba SC) na Peter Manyika (Singida United).

Walinzi ni Gadiel Michael (Young Africans), Boniphace Maganga (Mbao FC), Kelvin Yondani (Young Africans), Kennedy Juma (Singida United), Erasto Nyoni (Simba SC) na Mohammed Hussein (Simba SC).

Viungo wa kati ni Himid Mao ambaye ni Nahodha (Azam FC), Jonas Mkude (Simba SC), Hamis Abdallah (Sony Sugar/Kenya), Mzamiru Yassin (Simba SC), Raphael Daud (Young Africans), Shizza Kichuya (Simba SC), Abdul Hilal (Tusker/Kenya), Ibrahim Ajib (Young Africans) na Amani Kiata  wa Nakuru All Stars ya Kenya.

Washambuliaji ni Mbaraka Yussuph (Azam FC), Elias Maguri (Dhofar/Mascat, Oman), Daniel Lyanga (Fanja FC/Mascat), Yohana Mkomola (Ngorongoro Heroes) na Yahya Zayd kutoka Azam FC ya Dar es Salaam.

Benchi la Ufundi linaundwa na yeye Ninje ambaye ni Kocha Mkuu mwenye Daraja ‘A’ la Shirikisho la Mpira wa Miguu Ulaya (UEFA), Fulgence Novatus (Kocha Msaidizi), Patrick Mwangata (Kocha wa Makipa), Danny Msangi (Meneja), Dkt. Richard Yomba (Daktari wa timu), Dkt. Gilbert Kigadye (Daktari wa Viungo) na Ally Ruvu (Mtunza Vifaa).

Katika michuano hiyo inayotarajiwa kuanza Desemba 3, mwaka huu, Kilimanjaro Stars imepangwa Kundi ‘A’ pamoja wenyeji Kenya, Rwanda na Libya ambayo ni timu mwalikwa kutoka Kaskazini mwa Afrika.

Kilimanjaro Stars ambayo imewahi kutwaa mara tatu taji hilo la Chalenji tangu kuanzishwa kwake, itaanza kampeni za kurudisha heshima yake dhidi ya Libya katika kundi hilo la A utaofanyika Desemba 3, mwaka huu.

Mashindano ya mwaka huu CECAFA ilifikia makubaliano na kanda mbili za Kusini mwa Afrika – COSAFA na ile ya Kaskazini UNAF kualika timu mbili za kutoka kanda hizo na mataifa ya Libya na Zimbabwe ambayo imejitoa.

Jumla ya timu shiriki kwenye CECAFA Senior Challenge Cup mwaka huu sasa tisa ambazo ni pamoja na wenyeji Kenya, Uganda, Tanzania, Rwanda, Burundi, South Sudan, Ethiopia, Zanzibar, Somalia na Libya.

Sudan wenyewe wamejiondoa katika mashindano ya mwaka huu wakati mataifa mawili ya Eritrea na Djibouti nayo hayatashiriki.

Michuano hiyo itatumia viwanja vya Moi kilichopo Kisumu (Moi Stadium), Bukungu kilichopo Kakamega na Afraha kilichopo Nakuru wakati Uwanja wa Kasarani Nairobi na ule wa Kenyatta uliopo Machakos vitatumika kama viwanja vya ziada.

Ratiba ya michuano hiyo mwaka huu ni kama ifuatavyo:

Desemba 3, 2017

Kundi A

Libya vs Tanzania

Kenya vs Rwanda

Desemba 4, 2017

Kundi B

Burundi vs Ethiopia

Desemba 5, 2017

Kundi A

Zanzibar vs Rwanda

Kenya vs Libya

Desemba 6, 2017

Kundi B

Uganda vs Burundi

Desemba 7, 2017

Tanzania vs Zanzibar

Rwanda vs Libya

Desemba 8, 2017

Kundi B

Sudan Kusini vs Ethiopia

Desemba 9, 2017

Kundi A

Rwanda vs Tanzania

Kenya vs Zanzibar

Desemba 10, 2017

Kundi B

Sudan Kusini vs Burundi

Ethiopia vs Uganda

Desemba 11, 2017

Kundi A

Libya vs Zanzibar

Kenya vs Tanzania

Desemba 12, 2017

Kundi B

Uganda vs Sudan Kusini

Desemba 13, 2017

Mapumziko

Desemba 14, 2017

Nusu fainali 1 (Mshindi Kundi A vs Mshindi wa pili Kundi B)

Desemba 15, 2017

Nusu fainali 2 (Mshindi Kundi B vs Mshindi wa pili kundi A)

Desemba 16, 2017

Mapumziko

Desemba 17, 2017

Mshindi wa Tatu & Fainali

Wateuliwa Kuunda Kamati Ndogondogo AFCON U17
Airtel Tanzania yatoa msaada kwa Jeshi la Zimamoto