Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Bashiru Ally amesema kuwa mbunge wa jimbo la Mtama, Nape Nnauye na mbunge wa Nzega Mjini, Hussein Bashe ni watukutu ambao wanafaa kuongoza kampeni za ubunge wa chama hicho kwenye uchaguzi mdogo wa Jimbo la Buyungu.

Amesema kuwa wabunge hao ni watukutu na wakorofi wanaopenda kudadisi mambo hali ambayo huzua minong’ono mbalimbali ndani na nje ya CCM.

Dkt. Bashiru amesema kuwa kwa sasa CCM inapaswa kujivunia wabunge hao kutokana na namna wanavyodadisi mambo na kuyafuatilia, jambo linalofanya mawaziri wafikiri kwa kina kabla ya kutoa majibu na maamuzi.

Ameyasema hayo alipokuwa akizungumza na wanachama wa CCM alipopita wilayani Nzega wakati akielekea Kigoma kwenye kampeni za uchaguzi.

“Nawafahamu wabunge hawa kuwa ni watukutu kweli kweli, wadadisi kwelikweli, lakini wanapishana, kwa kuwa Nape ni mdadisi na mtukutu ambaye joto lake ni kali hivyo kazi yake ni kupooza,” amesema Dkt. Bashiru

Aidha, Wabunge wengine watakaoshiriki kwenye kampeni hizo ni Job Lusinde (Mtera), Martha Mlata (Viti Maalumu CCM), Munde Tambwe (Viti Maalumu CCM), Sixtus Mapunda (Mbinga Mjini), Jackline Ngonyani (Viti Maalum CCM).

Hata hivyo, ameongeza kuwa kutokana na udadisi wao na kile ambacho watu wengine wanaona kama ni utukutu, ilifikia wakati baadhi ya wanachama na watu ndani ya CCM walianza kutaka waondolewe, suala ambalo yeye hakubaliani nalo.

Leicester City wabuni mkakati wa kumzuia Harry Maguire
Samia Suluhu afungua kongamano la biashara na uwekezaji