Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Bashiru Ally amesema kuwa vyama vya siasa hapa nchini vinasumbuliwa na matatizo matatu kikiwemo chama chake, kuwa ni kutokuwa na mtazamo wa pamoja kiitikadi, nidhamu na utegemezi.

Ameyasema hayo Jijini Dar es salaam wakati akichangia mada katika mdahalo wa miaka 19 ya kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, ambapo mada kuu ilikuwa ni mienendo ya uchaguzi na mustakabali wa mataifa ya Afrika, ulioandaliwa na Kigoda cha Mwalimu Nyerere.

Amesema kuwa katika suala la kutokuwa na mtazamo wa pamoja wa kiitikadi, chama kinapaswa kufahamu nini wanatakiwa kufanya, si kubishana wenyewe kwa wenyewe na hali hiyo ipo zaidi ndani ya CCM kuliko vyama vingine.

Aidha, amesema nidhamu ni moja ya matatizo aliyokumbana nayo ambapo kwa ujumla wake alisema vyama vingi havina nidhamu.

“Vyama vyetu havina nidhamu kwanza hawahudhurii vikao, pia wana matumizi mabaya ya fedha, wengine ni waheshimiwa lakini ni wezi, kuna mmoja siwezi kumtaja kwa jina nilimkamata na gari la wizi nikamwambia ashuke japokuwa ni mbunge, ninawaomba fedha za usajili zitumike vizuri si mzigombanie,” amesema Dkt. Bashiru.

Hata hivyo, suala la tatu ambalo amelizungumzia katika mdahalo huo ni utegemezi ambapo amesema vyama vingi havina vyanzo vya ndani hivyo kuvifanya kuwa tegemezi.

 

Dkt. Mpango adai marekebisho ya sheria ya Takwimu hayana tatizo
Aaron Ramsey bado kizungumkuti Arsenal