Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani, amefanya ziara mkoani Katavi kwa lengo la kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa kwa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), mwaka 2017 ya kukamilisha ufungaji wa mitambo mipya ya kuzalisha umeme katika wilaya ya Mpanda  na Mlele mkoani humo.

Dkt. Kalemani alitoa maagizo hayo baada ya mitambo iliyokuwepo  katika kituo cha Mpanda kuharibika na hivyo kupelekea mkoa huo kuwa na changamoto ya upatikanaji wa umeme huku baadhi ya maeneo katika wilaya ya Mlele yakipata umeme kutoka nchini Zambia.

Meneja Miradi kutoka TANESCO, Stephen Manda alimweleza Dkt Kalemani kuwa,  ufungaji wa mitambo ya umeme katika kituo cha Mpanda umekamilika na sasa kituo kinazalisha umeme wa kiasi cha megawati 2.5 huku matumizi ya wilaya ya Mpanda yakiwa ni megawati 2.3.

Manda alieleza kuwa, kukamilika kwa mitambo ya umeme katika kituo cha Mpanda  kumewezesha vijiji 14 kusambaziwa umeme ikiwemo wilaya mpya ya Tanganyika ambayo imepata umeme kwa mara ya kwanza kutoka kuanzishwa kwake.

Akiwa katika wilaya ya Mlele, Dkt. Kalemani alielezwa kuwa, ufungaji wa mashine moja ya kuzalisha umeme yenye uwezo wa kilowati 476 umekamilika na kuwezesha baadhi ya wakazi wa Mlele hususan Makao Makuu ya wilaya hiyo (Inyonga) kupata umeme.

Baada ya kupata taarifa ya utekelezaji wa maagizo yake,  Dkt Kalemani aliwapongeza wataalam wa TANESCO waliosimamia na kutekeleza kazi hiyo ndani ya wakati uliopangwa.

Aidha, alitoa maagizo kwa TANESCO ya kuongeza mitambo mingine miwili ya uzalishaji umeme katika kituo cha Mpanda na mmoja katika kituo cha Inyonga wilayani Mlele ili kuweza kuwa na umeme wa kutosha utakaowezesha wanannchi kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo uanzishaji wa Viwanda.

Kwa kuwa mitambo hiyo  inatumia mafuta kuzalisha umeme, Dkt Kalemani alisema kuwa, Serikali ipo kwenye maandalizi ya kuanza ujenzi wa miundombinu ya kusafirisha umeme kwa msongo wa kV 400 kutoka mkoani Mbeya- Sumbawanga-Katavi – Kigoma hadi Nyakanazi. Hivyo mkoa wa Katavi utapata umeme wa gridi ya Taifa na kuachana na mitambo ya mafuta ambayo inatumia gharama kubwa.

Akizungumza na wananchi wilayani Mlele, Dkt Kalemani aliwaasa kujitokeza kwa wingi ili kuunganishwa na huduma ya umeme na hivyo kujiletea maendeleo huku akitolea mfano wilaya ya Mlele ambayo matumizi yake ya umeme ni kW 71 ambayo ni sawa na asilimia 15 tu ya uwezo wa mtambo.

Mkuu wa mkoa wa Katavi, Meja Jenerali (Mst), Raphael Muhuga alimshukuru Waziri wa Nishati kwa kutoa maagizo ya kufunga mashine nyingine tatu mpya za kufua katika  mkoa wa Katavi suala ambalo litapelekea mkoa huo kuwa na umeme wa uhakika.

Vilevile aliisisitiza Wizara kuharakisha utekelezaji wa mradi wa umeme wa kilovolti 400 ambao kukamilika kwake kutafungua fursa za kiuchumi mkoani humo kutokana na kuwa na umeme wa kutosha na wa uhakika.

Katika ziara hiyo,  Waziri Kalemani aliambatana na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakala wa Nishati Vijijini, Dkt. Gidion Kaunda na Mwenyekiti wa Bodi ya TANESCO, Dkt. Alexander Kyaruzi ambao kwa nyakati tofauti waliwaasa wananchi kulinda miundombinu ya Umeme ili kutorudisha nyuma juhudi za Serikali za kusambaza umeme nchini.

Mhagama atoa ufafanuzi muungano wa mifuko ya pensheni
Mutungi aingilia kati kampeni za uchaguzi Siha, Kinondoni