Baraza la Sanaa la Taifa (Basata) limemfungulia Godfrey Tumaini maarufu kama Dudu Baya, baada ya kusamehewa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe.

Baraza hilo limetangaza uamuzi wa kumfungulia leo, Februari 12, 2020 baada ya kumfungia kwa kipindi kisichojulikana tangu mwaka jana kwa kile ilichoeleza kuwa amekiuka maadili kwa maneno aliyoyasema kwenye mitandao ya kijamii.

Katibu Mtendaji wa Baraza hilo, Godfrey Mngereza amesema kuwa Dudu Baya alikata rufaa kwa Waziri Mwakyembe, kama inavyoelekeza Sheria iliyounda Baraza hilo. Alisema kuwa Waziri alimsikiliza na kumsamehe, hivyo kwa mujibu wa sheria hiyo Baraza pia linamtoa kifungoni.

“Sheria ya Baraza namba 23 ya Mwaka 1984 pamoja na marekebisho yake yaliyofanywa mwaka 2006 inaeleza kuwa mtu yeyote akipewa adhabu na Baraza anaweza kukata rufaa kwa Waziri; na atakachosema Waziri ndicho kitakachotekelezwa,” amesema Mngereza.

Amewataka wasanii kuhakikisha wanaishi kwa kuzingatia maadili kwakuwa wao wana nguvu kubwa kwenye jamii na wanafuatiliwa na watu wa rika zote ikiwa ni pamoja na watoto.

Awali, Dudu Baya alifika katika Ofisi za Baraza hilo Januari 23 mwaka huu kwa lengo la kusajiliwa, lakini alikataliwa. Baada ya uamuzi huo aliwasilisha malalamiko yake Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Dudu Baya ni moja kati ya wasanii wakongwe waliowahi kufanya vizuri sio tu kwa wimbo mmoja mmoja bali pia kwa Albam zao. ,Moja kati ya Albam zake zilizowahi kufanya vizuri ni ‘Papo kwa Papo’ aliyoitoa mwaka 2004.

Joseph Shabalala mkali wa miondoko ya kizulu afariki dunia
Mfanyabiashara apigwa faini mil.9 kwa kukosa mashine ya EFD