Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe ameyataka mashirikisho ya Sanaa na Filamu kusimamia ubora wa kazi za sanaa ili kukidhi mahitaji ya walaji.

Ameyasema hayo hii leo jijini Dar es salaam wakati akizungumza na viongozi wa Mashirikisho hayo ofisini kwake ambapo amewataka kusimamia ubora wa kazi zao kwani ndio kitu pekee kitawafanya mashabiki kuzipenda filamu za nyumbani.

“Ongezeni juhudi katika kusimamia uboreshaji wa kazi za sanaa na filamu ili ziweze kuthaminiwa na kukidhi matakwa ya walaji kwa kuwafanya kupenda vya kwetu,”amesema Dkt. Mwakyembe

Aidha, kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu Tanzania, Joyce Fisoo ameyataka Mashirikisho ya sanaa na filamu kufuata na kusimamia sheria, kanuni na taratibu za kutafsiri kazi za filamu za nje kwa kuwa na kibali cha mmiliki wa filamu.

Naye Kaimu Mkurugenzi Idara ya Maendeleo ya Sanaa, Leah Kihimbi, ameyaasa mashirikisho ya Sanaa na Filamu nchini kusimamia vyema vyama vilivyopo chini ya mashirikisho hayo ili kuhakikisha shughuli zote za sanaa zinapita kwenye mashirikisho husika.

TRA yakamata madumu 500 ya mafuta kwa kukwepa kodi
Shonza awataka waandishi wa habari kuzingatia maadili