Eliud Kipchoge amekuwa mtu wa kwanza katika historia ya mbio za marathon kukimbia kilomita 42 kwa muda wa chini ya saa mbili.

Raia huyo wa Kenya alikimbia muda wa kilomita 42.2 katika saa moja dakika 59 na sekunde 40 katika shindano la Ineos Challenge mjini Vienna nchini Austria siku ya Jumamosi.

Haitatambulika kuwa rekodi mpya ya dunia katika mbio hizo kwa kuwa halikuwa shindano la kila mtu mbali na kwamba alitumia kundi la wanariadha wa kusukuma kasi waliokuwa wakishirikiana naye na kutoka.

Alipogundua kwamba alikuwa anakaribia kuweka historia , wanariadha waliokuwa wakidhibiti kasi ya mbio hizo walirudi nyuma na kumwacha bingwa huyo kutimka hadi katika utepe huku akishangiliwa na mashabiki wengi mji mkuu wa Austria.

Bingwa huyo mara nne wa London Marathon alimkumbatia mkewe, akachukua bendera ya Kenya na kukumbatiwa na wanaridha waliokuwa wakimsaidia kuweka muda huo bora wakiwemo mabingwa katika mbio ndefu duniani.

Kipchoge, aliyelinganisha mbio hizo na mtu wa kwanza kwenda mwezini kabla ya kuanza kukimbia alisema kwamba ameweka historia sawa na raia wa Uingereza Sir Roger Bannister alivyofanya wakati alipokweka muda bora 1954.

”Nahisi vyema, baada ya Roger Bannister kuweka historia ilinichukua miaka 65 . Nimejaribu lakini nimevunja”, alisema .Kipchoge

”Hii inaonyesha uzuri wa michezo. Nataka kuufanya mchezo huu kuwa safi na wa kufurahisha. Pamoja tunapokimbia tunafanya ulimwengu kuwa mzuri wa kuishi”.

Huku gari linalomuongoza likiwasha taa za rangi ya kijani katika barabara ili kuonyesha kasi anayotarajiwa kuweka ya dakika 2:50 kwa kila kilomita atakayokimbia, Kipchoge hakukimbia chini ya dakika mbili sekunde 52.

Ili kuweka muda huo, alilazimika kukimbia mita 100 katika sekunde 17.08 mara 422 mfululizo kwa kasi ya kilomita 21.1 kwa saa

Alikuwa sekunde 10 mbele ya mpangilio kufikia kilomita 21 , kabla ya kuonekana akipunguza kasi katika kilomita 2:52, na baadaye kuongeza kasi hiyo na kutimka mbio katika awamu ya mwisho.

Kipchoge alisaidiwa na kundi la wadhibiti kasi 42 akiwemo bingwa wa Olimpiki Matthew Centrowitz, mshindi wa medali ya shaba katika mbio za mita 5000 Paul Chelimo na ndugu wa Ingebrigsen Jakob , Filip na Henrik.

Walibadilishana zamu mara kwa mara , wakikimbia huku wamemzunguka Kipchoge huku naye bingwa wa zamani wa mbio za mita 1500, na 5,000 Bernard Lagat akimuongoza katika kilomita ya mwisho.

”Ni miongoni mwa wanariadha bora duniani hivyo basi ahsante na nawashukuru kwa kukubali kazi hii tulifanikiwa pamoja”alisema.

Wakufunzi wa Kipchoge walimpatia maji kwa kutumia baiskeli badala ya kuchukua vinywaji kama ilivyo kawaida kutoka katika meza zilizowekwa kandokando.

Usaidizi kama huo hauruhusiwi chini ya sheria za IAAF , na ndio maana shirika hilo la riadha duniani halitaitambua rekodi hiyo kama rekodi rasmi ya marathon.

Bingwa huyo wa Olimpiki alikuwa ameikosa rekodi hiyo na sekunde 25 katika jaribio lake la hapo awali 2017.

Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Oktoba 13, 2019
Kishindo cha JPM, Ahamia rasmi Dodoma