Serikali ya Zambia imepiga marufuku kinywaji cha kuongeza nguvu (energy drink) baada ya kubainika kuwa vimewekewa vitu vinavyoongeza nguvu za kiume na kuongeza mihemko ya kingono kwa wanaume mfano wa Viagra.

Kwa mujibu wa taarifa ya Serikali ya nchi hiyo, uamuzi huo umefikiwa baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa Taasisi ya Kusimamia Madawa ambayo ilibainisha kuwa kinywaji kiitwacho SX kina virutubisho vilivyochanganywa na Viagra.

Kinywaji hicho kinachotengenezwa na Kampuni ya Revin Zambia Ltd kinauzwa katika nchi kadhaa za Afrika kama Uganda, Malawi na Zimbabwe, Desemba 28 mwaka jana kililalamikiwa na mteja mmoja mwanaume ambaye alidai kuwa alijikuta akiwa na hamu/mihemko ya ngono kwa takribani saa sita mfululizo huku akitokwa na jasho jingi.

Serikali imeagiza kiwanda hicho kuondoa bidhaa hiyo sokoni  na kusitisha kabisa uzalishaji wake mara moja.

“Matokeo ya uchunguzi uliofanywa na Zimbabwe na Afrika Kusini pia umeonesha matokeo sawa kuwa kuna kila dalili kinywaji hicho kina dawa aina ya Sildenafil Citrate ambazo ni kama Viagra,” imeeleza taarifa ya Mamlaka ya eneo la Ndola nchini Zambia.

Mapema mwezi Januari, Malawi ilipiga marufuku kichwaji hicho baada ya kufanyika uchunguzi katika ubora wa virutubisho vilivyowekwa kwenye kinywaji hicho.

Kinywaji hicho ambacho jina lake kwa urefu ni Natural Power Energy Drink SX ni maarufu sana nchini Zambia hususan kwa wanaume na inauzwa katika ujazo wa mililita 500, katika bar na maduka makubwa.

Burundi: Wanafunzi wakamatwa kwa kuharibu picha ya Rais
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Machi 22, 2019