Kocha wa timu ya taifa ya Urusi, Leonid Viktorovich Slutsky, amemjumuisha beki wa klabu ya Schalke 04, Roman Neustadter kwenye kikosi chake ambacho kitashiriki fainali za Euro 2016, nchini Ufaransa.

Neustadter amtejwa kwenye kikosi cha Urusi, huku uraia wake ukiwa na utata kufuatia kuwa na uzawa na nchini Ukraine na mpaka sasa bado hajapata uthibitisho wa uraia wa nchini Urusi.

Beki huyo mwenye umri wa miaka 28, amekua akiishi nchini Ujerumani tangu akiwa na umri mdogo, na tayari ameshawahi kuitumikia timu ya taifa ya vijana ya nchi hiyo ambayo iliibuka mabingwa wa dunia katika fainali za kombe la dunia za mwaka 2014 zilizochezwa nchini Brazil.

Hata hivyo, taarifa kutoka ndani ya shirikisho la soka nchini Urusi zinadai kwamba, Neustadter anatarajia kukabidhiwa hati yake ya kusafiria ya nchi hiyo (Passport) wakati wowote juma hili, hatua ambayo itamtambulisha rasmi kama raia.

Katika hatua nyingine aliyekua mshambuliaji wa pembeni wa klabu ya Chelsea Yuri Zhirkov, ambaye kwa sasa anaitumikia Zenit St Petersburg, pamoja na mfungaji bora wa muda wote kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Urusi Alexander Kerzhakov, wameachwa katika kikosi kitakachoshiriki fainali za Euro 2016.

Zhirkov, ameshindwa kuitwa katika kikosi hicho kufuatia majeraha ya kisigino yanayomsumbua kwa sasa, huku Kerzhakov mwenye umri wa miaka 33, akiachwa kwa sababu za kushindwa kuonyesha umahiri wake wa soka tangu alipopelekwa kwa mkopo kwenye klabu ya FC Zurich ambayo imemaliza katika nafasi ya mwisho kwenye ligi ya nchini Uswiz.

Kerzhakov, alipelekwa kwa mkopo nchini Uswiz, baada ya kukosa sehemu ya kwanza ya msimu wa soka nchini Urusi kufuatia majeraha yaliyomuweka nje kwa muda mrefu, na alipopata ahuweni meneja wa klabu ya Zenit, Andre Villas-Boas alichukua uamuzi wa kumpeka nje ya ligi ya nchini Urusi kwa kuamini angefanikiwa kurejesha uwezo wake wa soka.

Kikosi kamili cha timu ya taifa ya Urusi kilichotajwa kwa ajili ya fainali za Euro 2016 upande wa makipa yupo  Igor Akinfeev (CSKA Moscow), Guilherme (Lokomotiv Moscow) na Yuri Lodygin (Zenit St Petersburg).

Mabeki: Alexei Berezutski (CSKA Moscow), Vasili Berezutski (CSKA Moscow), Sergei Ignashevich(CSKA Moscow), Dmitri Kombarov (Spartak Moscow), Roman Neustadter (Schalke 04), Georgi Schennikov (CSKA Moscow), Roman Shishkin (Lokomotiv Moscow), Igor Smolnikov (Zenit)

Viungo: Igor Denisov (Dynamo Moscow), Alan Dzagoev (CSKA Moscow), Denis Glushakov (Spartak Moscow), Alexander Golovin (CSKA Moscow), Oleg Ivanov (Terek Grozny), Pavel Mamaev (Krasnodar), Alexander Samedov (Lokomotiv Moscow), Oleg Shatov (Zenit St. Petersburg) na Roman Shirokov (CSKA Moscow)

Washambuliaji: Artem Dzyuba (Zenit St. Petersburg), Alexander Kokorin (Zenit St Petersburg) na Fedor Smolov(Krasnodar).

Timu ya taifa ya Urusi, umepangwa katika kundi la pili (B) sambamba na England, Slovakia pamoja na Wales.

Ryan Giggs Kuondoka Old Trafford
CCM yatoa tamko kuhusu Kitwanga na kama itamuadhibu tena