Mipango ya kukabiliana na “tabia isiyovumilika” ya wachezaji na mameneja katika soka la England imetangazwa. Katika taarifa iliyotolewa na Ligi Kuu, Ligi nyingine na Chama cha soka cha England, imesema nidhamu mbaya imefikia “viwango visivyokubalika”.

Kuanzia msimu huu, kadi nyekundu zitatolewa kwa wachezaji watakaomkabili mwamuzi au kutumia lugha za matusi au hata kwa ishara.

Nidhamu pia katika ‘benchi la ufundi’ itazingatiwa. Hakuna mchezaji hata mmoja katika Ligi Kuu ya England alioneshwa kadi nyekundu kwa kumtukana au kutumia lugha chafu kwa mwamuzi katika misimu mitano iliyopita.

Lakini mwenyekiti wa Ligi Kuu, Richard Scudamore amesema kumekuwa na wasiwasi “kwa muda sasa” kuwa wachezaji wamekuwa “wakivuka mipaka”.

“Kwa pamoja tumeona tabia hii haitakiwi kuendelea kuvumiliwa,” amesema Scudamore. “Matukio yanatokea kwa haraka sana kwenye mchezo wenye mvutano mkali. Bado tunataka kuona ari ambayo mashabiki watafurahia, lakini wachezaji na mameneja watatakiwa kuwa makini kuwa hawavuki mipaka.”

Makosa yanayoweza kusababisha kadi ya manjano:

Kuonesha nidhamu mbaya waziwazi kwa mwamuzi yoyote;

Kubishia uamuzi kwa ghadhabu;

Kumkabili mwamuzi uso kwa uso;

Kumkimbilia mwamuzi kubisha kuhusu uamuzi uliotolewa;

Lugha ya matusi, lugha chafu au ishara za matusi dhidi ya waamuzi;

Kumgusa mwamuzi yoyote bila ya ghadhabu kupinga uamuzi;

Kadi ya manjano kwa angalau mchezaji mmoja pale mchezaji mmoja au zaidi watamzonga na kumzunguka mwamuzi.

Makosa ya kadi nyekundu:

Iwapo mchezaji atamkabili mwamuzi na kutumia lugha ya matusi au kutumia ishara.

Kumgusa mwamuzi kwa ghadhabu kupinga uamuzi.

Video: Naibu Waziri Atoa Wito Huu Kwa Watanzania
Kufungiwa kwa Wimbo Kunamrudisha Msanii Nyuma- Shaa