Mamlaka ya safari za Anga Tanzania (TCAA), imetangaza kuwa kampuni ya ndege ya Fastjet imepoteza sifa za kufanya biashara nchini. TCAA imetoa notisi ya siku 28 ya kusudio la kusitisha leseni ya kampuni ya kutoa huduma za usafiri wa anga Tanzania.

Hayo yamesemwa jijini Dar es salaam na Mkurugenzi Mkuu wa TCAA, Hamza Johari ambapo amesema kuwa kwa sasa wameamua kuwapa notisi ya siku 28 ili waweze kujipanga upya kama wanaweza kuendelea na biashara au imeshawashinda kutokana na mwenendo mzima wa biashara wanavyoiendesha.

Amesema kuwa Fastjet imepoteza sifa ya kufanya biashara nchini, na wameizuia ndege moja waliyonayo kuruka kutokana na matatizo ya mara kwa mara na kukosekana kwa meneja mwajibikaji wa shirika.

“Tumekuwa tukiwaandikia barua ya kuwataka watueleze kuhusu mwenendo wao wa biashara tangu Fastjet Plc wajiondoe lakini pia shirika limekuwa na madeni mbalimbali ambayo hayajalipwa. Tukiomba watupe mpango wao wa fedha na biashara kwa mujibu wa sheria hawafanyi hivyo,” amesema Johari.

Aidha, amesema shirika hilo linadaiwa na watoa huduma wake wengi ikiwemo TCAA inayolidai Sh1.4 bilioni lakini pia halina meneja mwajibikaji ambaye ni mtaalamu wa masuala ya ndege anayepaswa kutoa majibu ya hali ya ndege.

Hata hivyo, amewaomba wananchi kuepuka kutapeliwa na wale watoa huduma watakao wakatia tiketi za Fastjet wakati hazifanyikazi kwa sasa, hawana ndege wameyumba.

Mapema leo FastJet imesimamisha safari zake zote na tayari imetangaza kuanzia Desema 20, kuwarudishia nauli kwa abiria waliokuwa wasafiri Disemba na Januari mwaka huu.

Mbunge alalamikia malipo kidogo ya Korosho
Serikali kuwakaanga wadanganyifu kwenye bima ya afya