Rais wa Chama Cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), Fatma Karume ameweka wazi sababu za kutowania tena nafasi hiyo katika uchaguzi ujao.

TLS inatarajia kufanya uchaguzi wa Rais, Aprili mwaka huu ikiwa ni mwaka mmoja baada ya kufanyika kwa uchaguzi huo. Fatma alipokea kijiti cha nafasi hiyo kutoka kwa Tundu Lissu, Wakili na Mbunge wa Singida Mashariki.

Fatma Karume amesema kuwa hataweza kushiriki katika uchaguzi huo mwaka huu kwani washirika wake katika biashara wanamhitaji.

“Ni kweli sitoshiriki. My partners want me to dedicate my time in our business (washirika wangu wanataka nitumie muda wangu kwenye biashara yetu),” Fatma aliiambia Nipashe.

Fomu za uchaguzi huo zimeshachukuliwa na watu kadhaa wamejitokeza kuwania nafasi hiyo, huku jina la Fatma likikosekana kwenye orodha ya majina hayo.

Wakili huyu msomi, ameandika historia ya kuwa mwanamke wa kwanza kuwa Rais wa TLS tangu kuanzishwa kwake mwaka 1954.

Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Februari 19, 2019
Polisi aliyetoa amri 50 Cent apigwe risasi kusomeshwa namba