Mabingwa wa soka nchini Hispania FC Barcelona huenda wakamuweka sokoni mshambuliaji wa pembeni kutoka nchini Ufaransa Ousmane Dembele, itakapofika wakati wa usajili wa majira ya baridi mwezi Januari 2019.

Taarifa kutoka ndani ya klabu hiyo ya Cataluña zinaeleza kuwa, Dembele amekua mtovu wa nidhamu, tofauti na alivyokua anachukuliwa klabuni hapo, baada ya kusajiliwa msimu uliopita akitokea Borussia Dortmund ya Ujerumani kwa ada ya Pauni milioni 96.

Mshambuliaji huyo anadaiwa kuchelewa kujiunga na wenzake kabla ya mchezo wa ligi ya mabingwa barani Ulaya dhidi ya Inter Milan uliochezwa juma lililopita, na matokeo yake alifika uwanjani dakika 25 kabla ya mpambano huo kuanza.

Kitendo hicho kinadaiwa kumuudhi meneja wa FC Barcelona Ernesto Valverde, ambaye ameutaka uongozi kutafuta mbinu za kumuondoa Dembele kikosini kwake.

Hata hivyo, pamoja na kutao agizo hilo kwa uongozi, bado Valverde alimtumia Dembele kwenye mchezo wa ligi dhidi ya Real Madrid (El Clasico) mwishoni mwa juma lililopita, kabla ya kumtoa na nafasi yake kuchukuliwa na Arturo Vidal.

Tayari klabu tatu zinazoshiriki ligi kuu ya soka nchini England Chelsea, Arsenal na Liverpool, zinatajwa kumuwania mshamnbuliaji huyo mwenye umri wa miaka 21.

Dembele ambaye alikua sehemu ya kikosi cha Ufaransa kilichotwaa ubingwa wa dunia mwaka huu, tayari ameshaitumikia FC Barcelona katika michezo 27 na kufunga mabao sita.

Dele Alli kubaki Spurs hadi 2024
Ukeketaji wahamia kwa vichanga