Kampuni ya uchunguzi na utafiti wa madini, Helium One imegundua kuwapo kwa futi za ujazo bilioni 98.9 za gesi katika maeneo mbalimbali iliyoyafanyia utafiti mkoani Rukwa.

Hayo yamesemwa hii leo katika warsha ya siku moja iliyofanyika Chuo Kikuu cha Dar es salaam, na kuratibiwa na Idara ya Jiolojia ya chuo hicho, Helium One na Chuo Kikuu cha Oxford.

Akizungumza katika warsha hiyo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Helium One, Thomas Abraham-James amesema kuwa lengo la kuwa na warsha ni kuwaita wataalamu ili kuweza kubadilishana uzoefu na kutoa taarifa zilizopo kuhusu gesi hiyo pia kuangalia fursa mbalimbali.

“Helium One inaamini kwamba kuna fursa kupitia utafiti huu kuweza kutengeneza utaalamu wa kiwango cha juu na utaalamu wa hapa nchini juu ya uendelezaji wa gesi hiyo. Tutaendelea kujenga uhusiano na Chuo Kikuu cha Dar es salaam kuweza kubadilishana elimu, kutoa mafunzo kwa wanafunzi na maofisa wizara ya madini na kutengeneza mpango wa ufadhili wa masomo,” amesema James

Aidha, warsha hiyo imehudhuriwa na wanasayansi waandamizi wa gesi kutoka Chuo Kikuu cha Oxford cha Uingereza na Idara ya Jiolojia ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam (UDSM) watu wenye mamlaka na maamuzi, wadau wa maendeleo, watengeneza sera kutoka serikalini, watafiti na sekta binafsi.

Hata hivyo, Kampuni hiyo imetoa ufadhili wa masomo ngazi ya shahada ya uzamili kwa wanafunzi wawili wa UDSM kusoma katika Chuo Kikuu cha Oxford, ikiwa ni sehemu ya kuingiza utaalamu wa hali ya juu wa kisayansi kwa Watanzania na pia kuendeleza uhusiano mzuri kati ya Helium One na UDSM.

Wanafunzi wachomana visu kwa kubishania dini
Tanzia: Jaji Kisanga afariki dunia