Kocha Mkuu wa timu ya soka ya vijana wenye umri wa chini ya miaka 17 ya Shelisheli, Gavan Jeanne ameonesha kuihofia Serengeti Boys ya Tanzania katika mchezo wa kuwania nafasi ya kucheza fainali za Kombe la Mataifa utakaofanyika Juni 26, 2016 kuanzia saa 10.00 jioni kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Jeanne alionesha hofu hiyo leo Juni 25, 2016 alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari na mbele ya Kocha Mkuu wa Serengeti Boys, Bakari Shime ambao kwa pamoja walikuwa wakmizungumzia namna walivyoandaa timu zao kwa ajili ya mchezo huo wa kesho.

“Hatujawahi kushiriki michuano ya vijana. Hii ni mara yetu ya kwanza. Tumekuja kujifunza kwa wenzetu Tanzania ambao wana uzoefu,” alisema Jeanne ambaye pia alithibitisha kuwa hawajawahi kucheza mchezo wa kirafiki wa kimataifa.

Kwa upande wa Bakari Shime wa Serengeti Boys, alisema ameindaa mechi hiyo vema kiakili na kimwili kwa ajili ya kuikabili Shelisheli katika mchezo huo ambao hamasa yake imekuwa kubwa kwa kuwa kikosi hicho kinaandaliwa kuwa timu ya taifa baada ya miaka miwili.

Wachezaji wa Serengeti Boys wamesema, watafanya vema kwenye mchezo huo. Wachezaji hao ni Anthony Shilole ambaye alisema: “Tumejifunza mambo mengi, ushindi ni lazima kwa sababu tutafuata maelekezo ya walimu wetu. Tutajitahidi tushinde.”

Ally Ng’anzi: Maandalizi ni mazuri. Mechi ya Jumapili tumejiandaa vema. Tunashinda tena kwa magoli mengi.”

Ally Msengi: “Watanzania watarajie ushindi baada ya maandalizi ya muda mrefu. Timu iko kambini kitambo.”

Kennedy Nashony: Tutapambana kadiri ya uwezo. Kila mechi kwetu ni fainali. Hatuko tayari kupoteza ili kukosa mechi zijazo.”

Shelisheli ilitua Ijumaa usiku saa 7.45 usiku ikiwa na viongozi 25 na imefikia hoteli ya Southern Sun iliyoko katikati ya jiji la Dar es Salaam.

Waamuzi wanne kutoka Ethiopia, ndio watakaochezesha mchezo huo. Waamuzi hao ni Belay Tadesse Asserese ambaye ni mwamuzi wa kati wakati wasaidizi wake ni Tigle Gizaw Belachew upande wa kulia na Kinfe Yilma Kinfe upande wa kushoto huku mwamuzi wa akiba atakuwa Lemma Nigussie. Kamishna wa mchezo huo atakuwa ni Bester Kalombo.

Serengeti Boys ilikuwa kambini tangu Juni 14, 2016 kujiandaa na mchezo huo wa kufuzu fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika dhidi ya vijana wenzao wa Shelisheli utakaofanyika Juni 26, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam. Mchezo wa marudiano kati ya Serengeti Boys na Shelisheli utachezwa Julai 2, 2016 huko Shelisheli.

Katika kuajindaa na mchezo huo, Serengeti Boys ilifanya ziara India ambako walishiriki mashindano ya vijana ya Kimataifa yanayotambuliwa na FIFA (AIFF International Youth Tournament 2016) kabla ya kurudi na rekodi ya kupigiwa mfano si tu katika Tanzania na kwa nchi za Afrika Mashariki.

VIINGILIO YANGA NA TP MAZEMBE HIVI HAPA
Video: RC Paul Makonda amezisimamisha Kampuni nne