Chama cha Mapinduzi (CCM) kimeteua majina ya watakao gombea katika uchaguzi mdogo wa ubunge kwa tiketi ya chama hicho.

Majina hayo yametangazwa mara baada kumalizika kwa kikao cha Kamati Kuu Maalum ya Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) kilicho ongozwa na mwenyekiti wa chama hicho na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli.

Akitoa taarifa mara baada ya kumalizika kwa kikao hicho, Katibu wa Itikadi na Uenezi, Humphrey Polepole amewataja waliopitishwa ambapo ni pamoja na Pauline Philipo Gekul jimbo la Babati Mjini, James Kinyasi Millya jimbo la Simanjiro, Joseph Michael Mkundi jimbo la Ukerewe na Marwa Ryoba Chacha jimbo la Serengeti.

Aidha, Polepole ameongeza kuwa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) imesema kuwa Novemba 15 mwaka huu ndio mwisho wa kupewa dhamana kwa wabunge na madiwani kutoka vyama upinzani kujiunga na CCM.

Hata hivyo, ameongeza kuwa zoezi la uandikishwaji wanachama wapya linaendelea kwa mujibu wa taratibu za kawaida za chama.

 

 

 

 

Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Oktoba 31, 2018
Moto wa ajabu wateketeza kanisa, picha ya Yesu yasalia