Gwiji wa Klabu ya Chelsea Gianfranco Zola amerejea klabuni hapo kama meneja msaidizi, baada ya kuajiriwa kwa kutoka nchini Italia Maurizio Sarri.

Uongozi wa Chelsea umethibitisha kurejea kwa Zola mwenye umri wa miaka 52, ambaye aliitumikia klabu hiyo kama mchezaji kuanzia mwaka 1996 hadi 2003, huku akicheza michezo 312 na kufunga mabao 80.

Kwa kiasi kikubwa Zola aliinufaisha Chelsea wakati akiichezea klabuni hiyo, hali ambayo imeendelea kutumika kama kumbukumbu kwa kila shabiki ambaye amekua akiifuatilia kwa ukaribu The Blues.

“Ni kama ndoto kwangu, lakini sina budi kukubali kuwa ni hali halisi imetokea. Nimefurahi kurejea klabuni hapa kwa mara nyingine tena kama mtendaji wa benchi la ufundi, ninajua ni changamoto nyingine kwangu, lakini ninaamini kwa ushirikiano mkubwa nitakaoupata kutoka kwa meneja mkuu Maurizio Sarri tutafanikisha jambo na kufikia malengo.”

“Kwa niaba ya Sarri ninawaomba mashabiki na kila mdau wa Chelsea kutupa ushirikiano, ninaamini ikiwa hivyo tutakua wamoja na tutafanikisha kinachokusudiwa klabuni hapa kuanzia msimu ujao wa ligi. Ni bahati kubwa kwa Chelsea kuwa na meneja kama Sarri, ana historia nzuri katika medani ya soka, na mimi nimefurahi kuwa sehemu ya benchi lake la ufundi.” Amesema Zola.

Tangu Zola alipoondoka klabuni hapo mwaka 2003, amewahi kufanya kazi kama kocha wa timu timu ya vijana ya italia chini ya umri wa miaka 16, na baadae alirejea England kuzinoa klabu za West Ham, Watford na Birmingham City.

Pia aliwahi kuwa meneja wa klabu ya Cagliari ya nchini kwao Italia na Al-Arabi ya Qatar.

Diego Perotti AS Roma itapata mbadala mahiri wa Alison
Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Julai 19, 2018