Mshambuliaji kutoka nchini Ufaransa Olivier Giroud ameapa kupambana vilivyo ili kufanikisha hatua ya kusalia klabuni hapo kwa kipindi kirefu zaidi, tofauti na sasa ambapo inasemekana huenda akauzwa.

Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 32 amehojiwa na toviti ya Telefoot kuhusu uhakika wa kuondoka Stamford Bridge, itakapofikia mwezi Januari 2019.

Giroud amesema ni mapema mno kuanza kujihukumu kuhusu harakati za kuondoka klabuni hapo, hasa katika kipindi hiki ambacho Chelsea inafanya vizuri katika michuano yote wanayoshiriki.

Amesema maneno huenda yakawa yanavumishwa na vyombo vya habari, lakini anachokifahamu yeye kama mchezaji, kujituma, kuwajibika na kupambana ndio ngao kubwa ambayo itamuwezesha kusalia klabuni hapo kwa kipindi kirefu.

“Siwezi kuzuia maneno yanayosemwa dhidi yangu, katika kipindi hiki utasikia mambo mengi sana kuhusu usajili, jina lango likitajwa ni jambo la kawaida,”

“Ninaendelea kujihisi furaha hata kama sichezi katika kikosi cha kwanza cha Chelsea, lakini malengo yangu yapo moyoni, ninajua nitafanya nini hadi kumshawishi meneja ili niweze kufikia lengo ya kucheza mara kwa mara.”

“Ninaendelea kuwa mvumilivu kwa hali yoyote, ninajua wakati wangu utafika nitacheza katika kikosi cha kwanza, nipo Chelsea kwa ajili ya kucheza soka sio jambo lingine lolote.”

Alipoulizwa kuhusu kuondoka mwezi Januari alijibu, “Inawezekana ikatokea, lakini binafsi sitaki iwe hivyo, kususdio langu ni kucheza soka hapa kwa kipindi kirefu, ninafurahia maisha ya hapa.”

Giroud alisajiliwa na Chelsea mwezi Januari mwaka huu 2018 akitokea Arsenal, baada ya kusajiliwa kwa mshambuliaji kutoka nchini Gabon Pierre-Emerick Aubameyang.

Tangu alipojiunga na Chelsea, Giroud ameshacheza michezo 22 na kufunga mabao matatu.

Wapenzi watiwa mbaroni kwa kughushi cheti malipo ya korosho
AS Roma, AC Milan kupigana vikumbo usajili wa Benatia