Google imewafukuza kazi watu 48 wakiwemo maafisa 13 wakuu kutokana na tuhuma za unyanyasaji wa kingono tangu mwaka 2016.

Katika barua yake kwa wafanyakazi wake, mkurugenzi mkuu, Sundar Pichai amesema kuwa kampuni hiyo kubwa ya teknolojia imeamua kuchukua msimamo huo mkali ili kuweza kudhibiti tabia kama hizo ambazo sio za kawaida.

Barua hiyo inafuatia mara baada ya ripoti ya New York Times kwamba muasisi wa Android, Andy Rubin alipokea $ 90 m kama kitita cha kuondoka licha ya kukabiliwa na tuhuma za uzalilishaji wa kingono na utovu wa nidhamu.

Aidha, msemaji wa Rubin amekanusha taarifa hizo na kusema kuwa Rubin aliamua kuondoka Google mwaka 2014 na kuanzisha kampuni yake ya Teknolojia iitwayo Playground.

“Tunataka tuwahakikishie kwamba tunatathmini malalamiko yote kuhusu unyanyasaji wa kingono au utovu wowote wa nidhamu, tunachunguza na tunachukua hatua,”amesema msemaji wa Google Sam Singer.

Kwa mujibu wa ripoti ya New York Times, imesema kuwa wakurugenzi wawili wa Google, wameeleza kuwa aliyekuwa mkurugenzi mkuu mtendaji, Larry Page alimuomba Rubin kujiuzulu baada ya kampuni hiyo kuthibitisha malalamiko ya mfanyakazi mwanamke kuhusu tendo la ndoa lililofanyika katika chumba cha hoteli moja mnamo mwaka 2013.

 

Watoto wa chekechea wajeruhiwa vibaya na kisu
Video: Kamanda Sirro aibua jipya la Mo, Dawa za kulevya zatikisa shirika la Posta nchini