Askofu Josephat Gwajima amejibu tuhuma zilizoelekezwa kwake na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbroad Slaa kuwa alishiriki kama ‘mshenga’ kumshawishi mwanasiasa huyo kumpokea Edward Lowassa katika chama hicho.

Jana, Dk. Slaa alimtaja Askofu Gwajima kama mshenga na kwamba alimshawishi ampokee Lowassa huku akidai kuwa askofu huyo alimtamkia kuwa maaskofu 30 wa Kanisa Katoliki walihongwa na timu ya Lowassa.

Askofu Gwajima amekanusha taarifa zilizotolewa na Dk. Slaa ambaye alikuwa rafiki yake kwa muda mrefu akidai kuwa ni muongo mkubwa. Alisema kuwa Dk. Slaa ameamua kuwashambulia maaskofu hao kwa kuwa anafahamu hawana majukwaa ya kumjibu kama ilivyo kwa wanasiasa.

Gwajima alidai kuwa yeye aliitwa kama msuluhishi ndani ya Chadema na sio mshenga wa kumleta Edward Lowassa.

“Kwa kawaida inashangaza kwamba kama watu wawili wanagombana inatakiwa awepo mtu wa kuwaunganisha, ila anaposema maaskofu 34 haileti maana, haiingii akili, ameingiza Gwajima, Rostam Aziz na maaskfu,” Gwajima ameliambia gazeti la Mtanzania na kuongeza kuwa Dk. Slaa ametumwa na watu anaowafanyia kazi.

Askofu huyo alidai kuwa alichokisema jana Dk. Slaa kilikuwa silaha pekee ya CCM iliyokuwa imebaki na kuwataka waumini wake na watanzania kutoamini alichosema mwanasiasa huyo.

“Nafikiri Slaa ndio risasi ya mwisho ya mwisho iliyokuwa imebaki kwenye bunduki ya CCM,” alisema.

Jana Dk. Slaa alitangaza kustaafu siasa za vyama akieleza kutokana na kutoridhishwa na mwenendo wa siasa nchini hususani Chadema aliyoijenga kwa ajenda ya kupinga ufisadi na badala yake wamemkumbatia Lowassa waliyekuwa wanamtuhumu kuwa fisadi mkubwa.

Lescot Atimkia Aston Villa
Undani Wa Dk. Slaa Kuimwaga Chadema, Lowassa Na Kustaafu Siasa