Kada wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Methusela Gwajima amempongeza Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowasa kwa uamuzi wake wa kurudi CCM, na kuachana na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ambapo alikuwa Mjumbe wa Kamati Kuu.

Ametoa pongezi hizo mara baada ya Lowasa kupokelewa katika ofisi ndogo ya CCM Lumumba jijini Dar es salaam alipotangaza kuachana na CHADEMA na kurejea rasmi katika chama Mapinduzi alicho kitumikia kwa miaka mingi.

Amesema kuwa kitendo cha Lowasa kurudi CCM kinaonyesha ni namna gani kiongozi huyo alivyo na busara na moyo wa shukrani na jinsi alivyo na uwezo wa kupima mambo na kuzikubali kazi kubwa zinazofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM ,Dkt. John Pombe Magufuli.

”Nikweli hakuna ubishi hata wapinzani hili wanalijua kwamba Rais Magufuli amefanya mambo makubwa ya maendeleo na yenye maslahi makubwa kwa Taifa hili tangu aingie madarakani kiasi kwamba wapinzani sasa hawana jipya wamebaki kupinga tu hata mambo ambayo ni ya msingi na yenye maslahi kwa Taifa,”amesema Gwajima.

Hata hivyo, Gwajima ambaye kitaaluma ni mwanasheria amewaomba watanzania kuendelea kutii sheria bila shuruti kwa kujiepusha na vitendo vya uvunjifu wa amani, kuiunga mkono serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Magufuli na amewataka wanasiasa kutanguliza uzalendo kwa kila wanacho kisema na kukitenda badala ya maslahi yao binafsi.

 

Habari Picha: JPM aongoza maelfu ya wananchi jijini Dar es salaam kuaga mwili wa marehemu Ruge Mutahaba
Kangi Lugola aliliwa Kondoa, 'Baba tusaidie na hawa polisi'