Wakazi wa mtaa wa Jangwani na watumiaji wa barabara ya Morogoro road ambayo inapita maeneo ya Jangwani wamelazimika kutotumia barabara hiyo kutokana na kujaa kwa maji ambayo yanasababishwa na mvua zinazoendelea katika jiji la Dar es Salaam.

Wakizungumza watumiaji wa barabara hiyo wamesema serikali ingejaribu kutengeneza muinuko katika barabara hiyo kuanzia fire hadi Magomeni mapipa kusaidia kupunguza kero iliyopo kwasasa.

Pamoja na hivyo kuna baadhi ya vijana wanatumia mikokoteni pamoja na pikipiki kwaajili ya kuwavusha wananchi wanaokwenda mjini kwa gharama kubwa kuwahi kufanya shughuli zao.

“Nimetoka Gongo la Mboto kuja hapa kwaajili ya kuwavusha wananchi kuwahi makazini kwao, hii ni ajira kwangu hasa kutokana na baadhi ya wakazi wanaopita barabara hii kwenda makazini kwao inawalazimu kutafuta watu wa kuwavusha katika haya maji na uchafu uliopo katika barabara hii”. Amesema George Reonald ambaye anafanya kazi ya kuendesha bodaboda.

Vituo vya mwendokasi kuanzia kimara mpaka Magomeni vimejaa abiria kwa kukosa usafiri wa uhakika kutokana na majanga yaliyotokea jangwani hasa mabasi mengi ya mwendokasi kutokuweza kutoka katika sehemu ya kuyagesha magari hayo Jangwani.

Mariam Rashid ambaye pia ni mkazi wa magomeni amesema kuwa matatizo hayo yanasababishwa na wananchi wenyewe, hasa wengi wao kujaribu kutupa takataka ngumu katika miferiji na mito na kusababisha mitaro mingi kuziba na kutoruhusu maji yatembee.

Gwajima anazungumza na vyombo vya habari
LIVE: Yanayojiri Bungeni Jijini Dodoma