Kundi la wanariadha waliojawa na hasira limevamia makao makuu ya shirikisho la riadha nchini Kenya AK na kufunga milango wakilalamikia ubadhirifu na ufisadi katika jumba la Riadha mjini Nairobi.

Wanariadha hao waliwazuia maafisa wa shirikisho hilo la AK kuingia ofisini mwao.

Walikuwa wamebeba mabango ya kukashifu uongozi duni na ufisadi uliokithiri ofisini humo.

Maandamano hayo yanafuatia madai ya hivi karibuni kuwa takribani dola laki saba na nusu za Marekani ambazo ni za ustawishaji wa riadha nchini Kenya zililiwa na maafisa wakuu watatu wa shirikisho hilo.

Fedha hizo zilikuwa zimetolewa na kampuni ya kutengeneza bidhaa za michezo Nike.

Naibu mwenyekiti wa shirikisho hilo David Okeyo tayari anachunguzwa na idara ya kupambana na ufisadi.

Lakini Okeyo amekana madai hayo dhidi yake.

Vilevile wanariadha hao wanailaumu shirikisho hilo la Atheltics Kenya kwa kupokea hongo kutoka kwa mawakala wanaoshukiwa kuwashawishi wanariadha nchini humo kutumia madawa ya kutitimua misuli yaliyopigwa marufuku duniani.

Kenya ni moja ya mataifa yaliyotajwa kuwa na tatizo sugu la utumiaji wa dawa hizo za kuongeza nguvu mwilini na shirikisho la kupamabana na matumizi ya dawa hizo duniani WADA. 

Nikki Wa Pili: Lord Eyez Hafiki Ofisini Ndio Sababu Haonekani Kwenye Kazi Za Weusi
UEFA Champions League Kuendelea Leo