Halmashauri zote nchini zimehimizwa kuzingatia mipango bora wa matumizi ya ardhi ikiwemo  kuweka njia za Mifugo zitazowawezesha kwenda  kwenye Malisho, maji na kwenye Masoko Ili kuondokana na migogoro isiyo ya lazima baina ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi.

Rai hiyo ilitolewa na  Kaimu Mkuu wa Kitengo cha mazingira Wizara ya Mifugo na uvuvi  Sekta ya Mifugo, Yusuf Selenge katika mafunzo ya  ufugaji endelevu unaokabili mabadiliko ya tabia nchi yaliyofanyika Mkoani Geita.

Akiongea katika mafunzo hayo amesema kuwa  asilimia kubwa ya migogoro inatokana na baadhi ya vijiji kutokuwa na mipango ya matumizi bora ya ardhi na kusabisha njia za kupitisha mifugo ikitumika kwa matumizi mengine.

“Hii programu itasaidia sana kwa sababu imehimiza matumizi bora ya ardhi kwa hiyo Halmashauri wanatakiwa kutafuta wafadhiri na mapato yao ya ndani kuweza kutekeleza mpango huo kwa sababu njia za kupitisha mifugo zilikuwepo lakini zimevamiwa kwa matumizi mengine,” Amesema Yusufu.

Kuhusu mradi wa  utekelezaji wa mradi wa ufugaji endelevu,  Selenge amebainisha kuwa programu hiyo inatekelezwa katika sekta tatu za kilimo, mifugo na uvuvi ambapo kwa sasa mafunzo hayo yanatolewa kwa maafisa  katika Halmashauri ambao watawajibika kufikisha elimu kwa wakulima na wafugaji ngazi za vijiji.

“Halmashauri ndio wanachukua elimu hii na kuifikisha ngazi ya kata na kijiji, maafisa tunaofanya nao ni sita kwenye Halmashauri ambao ni Afisa  Mazingira, Afisa mifugo na uvuvi, Afisa kilimo na umwagiliaji, Afisa malisho, Afisa mipango pamoja na Afisa maendeleo ya jamii,” Ameongeza

Aidha Bw. Selenge amewahimiza  maafisa hao wa Halmashauri kuhakikisha wanawaelimisha  wafugaji njia bora ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi ikiwemo kuwashauri wananchi kuhimilisha Mifugo yao, kulima Malisho, kuyaboresha, kuyahifadhi, na kuvuna maji.

Naye, Afisa Mazingira kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Bw. Jeremiah Legela alisema kuwa pamoja na mambo mengine mafunzo hayo yatasaidia kuboresha mifugo ikiwemo kutoweka chapa katika mifugo ambayo imekuwa ikiharibu ngozi na kupunguza ubora.

Amesema mpango wa sasa ni kutumia njia ya kisasa ikiwemo kuweka hereni katika masikio na kuiacha ngozi ya mifugo zikiwa na ubora ambapo unahitajika katika soko hasa viwanda vya ngozi vilivyopo nchini.

Kwa upande wake, Afisa Mazingira wa Halmashauri ya Mji wa Geita, Bi. Mpelwa James  alibainisha kuwa faida waliyoipata katika mafunzo hayo watahakikisha inawafikia wafugaji ili kuhakikisha wanashiriki kulinda mazingira hasa katika vyanzo vya maji.

Hata hivyo hatua hiyo itawaongezea uelewa wananchi juu ya mabadiriko ya tabia ya nchi na itawajengea uwezo  wa kuhimili mabadiliko hayo ili waweze kuwa na uhakika wa kupata chakula cha mifugo na kwenye kaya zao kutokana na uzalishaji wenye tija.

Afisa mazingira kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Bw. Jeremiah Legela akiwasilisha mada kwa washiriki wa mafunzo ya namna ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi (hawapo pichani) yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Halmashauri ya mji wa Geita Mkoani Geita
Sehemu ya washiriki wa mafunzo ya namna ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Halmashauri ya mji wa Geita Mkoani Geita
Kaimu Mkuu wa kitengo cha mazingira Wizara ya Mifugo na Uvuvi, (Mifugo) Bw. Yusuf Selenge (wa nne kutoka kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya  watendaji wa Halmashauri ya geita mara baada ya mafunzo mafupi ya kuongeza uelewa wa kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi  kwa watendaji hao yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Halmashauri ya mji wa Geita Mkoani Geita

Mrembo Mtanzania aliyefungwa miaka 8 China atoka gerezani kwa Kishindo
Eric Omondi atiwa mbaroni