Baada ya kutangaza kuachia ngazi kwa kile kilichosemekana kutokushirikishwa katika maamuzi ya kuingia udhamini kati ya Simba na Kampuni ya Sportspesa, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe, ametangaza kutengua maamuzi yake ya kujiuzuru nafasi hiyo na Uenyekiti wa usajili na kurudi kwa ajili ya kuendelea na majukumu yake kama kawaida.
 
Aidha, Hans poppe amefikia maamuzi hayo mara baada ya kufanyika kwa kikao kilichochukua masaa kadhaa usiku wa kuamkia leo cha kujadili mambo mbalimbali kuhusiana na uamuzi wa kuingia udhamini na Kampuni hiyo.
 
Jana Mwenyekiti huyo wa Kamati ya usajili ya Simba alitangaza kujiondoa kwenye kamati ya utendaji na kubaki mwanachama wa kawaida ili kupisha kile ambacho alikiita sintofahamu ndani ya Klabu hiyo.
 
“Kweli tumekutana kikao kilianza mapema lakini tuliendelea kujadili mambo mbalimbali mpaka mida kama ya saa tisa usiku hivi, ndipo tulipokubaliana na tumeyamaliza vizuri na sasa tunasonga mbele,”amesema Hans Poppe.
 
Simba majuzi ilisaini mkataba wa miaka mitano na Kampuni ya Sportspesa wenye thamani ya shilingi bilioni 4.9 hivyo kusababisha baadhi ya viongozi kuingiwa na taharuki ya kile kilichotokea

Mtoto wa Osama atoa vitisho vipya kwa Marekani kuhusu kifo cha baba yake
Anaswa kwa kumuuza mtoto wake mwenye umri wa siku moja