Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF) limetangaza viingilio vya mchezo wa Jumatano kati ya Tanzania (Taifa Stars) dhidi ya Malawi (The Flames) kuwa ni shilingi elfu tano (5,000) katika mchezo huo wa kuwania kufuzu kwa fainali za kombe la Dunia mwaka 2018 nchini Urusi.

Viingilio vilivyotangazwa leo ni kiingilio cha juu kabisa kwa mchezo huo shilingi elfu kumi (10,000) kwa viti vya VIP B & C, huku viti vya rangi ya chungwa, bluu na kijani ikiwa ni shilingi elfu tano (5,000).

Stars inayonolewa na kocha mzawa Charles Boniface Mkwasa imeendelea kujifua katika viwanja vya Gymkhana na uwanja Taifa jioni kujiandaa mchezo huo wa Jumatano dhidi ya Malawi, huku wachezaji wakiwa wenye ari na morali ya hali ya juu kuelekea kwenye mechi hiyo.

Wachezaji 22 wapo kambini akiwemo mshambuliaji Mrisho Ngasa anayecheza soka la kulipwa nchini Afrika Kusini aliyeripoti jana mchana kambini, huku wachezaji wawili Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu wakitarajiwa kujiunga na wenzao leo wakitokea Lubumbashi – Congo DR.

Wakati huo huo timu ya Taifa ya Malawi (The Flames) imewasili nchini jana saa 4 asubuhi na kufikia katika hoteli ya De Mag iliyopo Mwanayamala, ambapo kikosi hicho leo kimefanya mazoezi asubuhi katika uwanja wa Boko Veterani.

Waamuzi wa mchezo huo kutoka nchini Somalia, kamisaa na mtathimin waamuzi wa wanatarajiwa kuwasili leo nchini na kufikia katika hoteli ya Protea iliyopo Oysterbay.

Mwamuzi wa kati ni Hagi Yabarow Wiish (Somalia), akisaidiwa na Hamza Hagi Abdi (Somalia), Salah Omar Abubakar (Somalia), mwamuzi wa akiba Bashir Olad Arab (Somalia), mtathimini wa waamuzi Sam Essam Islam (Misri) na kamisaa wa mchezo ni Muzambi Gladmore (Zimbabwe).

Floyd Mayweather Aendelea Kufanya Kufuru
Zlatan Ibrahimovic Amchakaza Pauleta