Ukiwa mmiliki wa kisima cha maji safi ya kunywa, tena pekee unachokitegemea huwezi kupuuzia kirahisi tetesi unazosikia mitaani za ‘mtoto wa jirani’ kuchafua maji hayo usipokuwepo. Hata kama utaonesha umepuuzia, kuna kitu unaweza kufanya ambacho kwa lugha ya kigeni wanasema ‘scanning the environment’.

Hivi karibuni kulizuka la kuzuka, yakawekwa mezani ya kuwekwa na wawekaji kuwa mlinzi binafsi wa Bosi wa WCB, maarufu kama Mwarabu Fighter anachafua maji ya kisima cha uhai wa moyo wa Harmonize. Eti kwamba, Mwarabu anachepuka kimyakimya na Sarah. Makubwa!!!

Harmonize na Sarah wakiangalia mechi ya Simba na Yanga, Uwanja wa Taifa

Hayo yalipata ‘kiki’ zaidi kwenye ukurasa wa Instagram wa Mange Kimambi ambao hata Mwarabu Fighter aliwahi kusema ndio ukurasa wa kwanza kuutembelea anapoamka asubuhi!

Tetesi hizo zilizowaacha wengi mdomo wazi, ingawa haziku-click kwenye kichwa cha Harmonize, zilimuamsha kusema jambo huku akimuwaza Sarah wake na kumuangalia kwa jicho la tatu Mwarabu Fighter ambaye amemtaja kuwa ni mwingi wa vitendo na adimu hata kutabasamu.

Mwarabu Fighter, Mlinzi wa Diamond

“Mara 10 ningesikia @mbosso_ anakula mzigo ningemsubiri pale @thelifeclub_1 tarehe 13/5/ na #kipanga yani ile anaingia tuu….!!! nikamuulia hapo hapo sasa mtu kama huyu hivi unaanzaje hata kumuuliza mana hata kucheka kwenyewe kwa msimu jamani Mungu huyu daah…..!!” Harmonize aliyaandika kwenye Instagram akimuweka ‘mtuhumiwa’ wake mwenye miraba minne.

Ingawa Harmonize aliiweka kiutani, mashabiki wake hawakuichukulia kama utani alioutaka, wengi waliishia kumshauri kama kweli ‘lisemwalo lipo na kama halipo laja’.

Ushauri uliomwagwa kwenye post hiyo unanikumbusha yaliyotokea baada ya kuzuka tetesi kuwa Beyonce wa Jay Z anachepuka na mlinzi wake binafsi, Julius De Boer. Ndiyo, yaani eti Queen Bey ameamua kuponea kwa mlinzi wake, ‘eti’ kwa sababu Jigga ameonekana anamuumiza kwa michepuko.

Ilianza kama utani uliopuuziwa karibu na kila mtu, lakini matokeo yake mwenye kisima chake, Jay Z aliamua kumtimua mlinzi huyo kimyakimya. Nieleweke vizuri, sipendekezi hii ifanyike kwa Mwarabu, kwanza Harmonize sio Bosi wake na tetesi zina mazingira tofauti.

Kama ya Sarah na Mwarabu Fighter yalivyoanza kwenye kurasa maarufu, sakata la kutikiswa kwa himaya ya Jigga kulianzia kwenye mitandao ya udaku.

Mitandao hiyo iliendelea kumwaga mchele kwenye kuku wengi, ikieleza zaidi hadi yaliyojiri ndani ya vyumba baada ya kuonekana nje. Huenda hii ndiyo iliyomshinda Jigga akaona bora kumuweka mbali mtuhumiwa wake asije kuwa kweli anachezea maji.

“Mwaka 2009, Beyonce mwenye umri wa miaka 32 alionekana akiwa anatoka hotelini akisindikizwa na Boer. Lips za Boer zilikuwa na rangi nyekundu ya lipstick anazotumia Beyonce,” ilieleza mtandao wa showbizspy.

Unaweza kujiuliza bila majibu, mitandao hii ilipata wapi hadi ya ndani ya nyumba? Wadaku wanajua wanavyodaka na kama wanayodaka ni ukweli mtupu au la.

Sakata hilo ingawa halikujibiwa kokote na Jigga wala Beyonce, kitendo cha kumpumzisha Boer kilikuwa ni sehemu ya majibu.

Mwisho wa siku, ingawa ukweli wa tetesi hizi huwa ni kizungumkuti, yaani haijulikani kama zimetungwa au la, huishia kusikojulikana kwenye akili ya wahusika wenyewe. Tunachoona kwenye mitandao kinaweza kuwa tofauti na kinachoendelea jikoni na ‘wazungu’ husema Vice Versa is True.

 

Nicki Minaj afichua siri, aitangaza tarehe yake
Burundi yatakiwa kuruhusu matangazo ya Redio