Aliyewahi kuwa mwenyekiti wa Klabu ya Simba, Hassan Dalali amewatupia dongo wapinzani wao wa jadi, Yanga kwa kusema kuwa ni kama pilipili hoho, kubwa lakini haiwashi.

Dalali alisema hayo mara baada ya kushuhudia Simba ikipata ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Uhuru, wikiendi iliyopita katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom.

Amesema kuwa wao hawana hofu juu ya Yanga kwa kuwa kwao si lolote na wao wapo tayari kuwafumua vibaya pindi watakapokutana.

Akiinadi timu yake zaidi, Dalali alisema: “Yanga ni kama nyanya ya Mchina, hawana lolote, nyanya ya Mchina inalika bwana.

“Simba usiifananishe na Yanga, kwanza Yanga wana njaa wanashindia mihogo, sisi tunaangalia mechi iliyo mbele yetu, wao Yanga wapo mbali, hatuwajali.

“Mimi nawajua Yanga vizuri, wao ni kama chapati ya maji isiyokuwa na vitunguu.”

Ikumbukwe kuwa Simba ipo katika mchakato wa kubadili aina ya mfumo wa uendeshaji wa klabu hiyo na mwanachama Mohamed Dewji ‘Mo Dewji’ ndiye ambaye aliyeshinda tenda ya kununua hisa kwa asilimia 41 mara baada ya mfumo huo wa mabadiliko kupita.

Zuma agoma kuachia madaraka
Mtoto amuua mdogo wake wa miaka 2 kwa risasi, ajiua